31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Ndugai, Abdallah Mwinyi wapenya uspika

mtz1*Naibu Mwansheria Mkuu naye apitishwa na CC

*Sitta atafakari sababu za kukatwa kwake, Dk. Nchimbi, Masaburi ‘Out’

NA DEBORA SANJA, DODOMA.

KAMATI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CC), imepitisha majina matatu ya wanachama wake waliomba kugombea  nafasi ya uspika  wa Bunge.

Majina yaliyopitishwa ni aliyekuwa Naibu Spika katika Bunge la 10, Job Ndugai, mtoto wa Rais mstaafu wa awamu ya pili, Abdullah Ali Mwinyi pamoja na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Tulia Akson.

Kupitishwa kwa majina hayo ya CC kunabakisha kazi ya wabunge wa CCM ambao watakutana leo mjini Dodoma na kuchagua jina moja ambalo litawasilishwa kwa Katibu wa Bunge, ambaye atakuwa mgombea uspika kupitia chama hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema katika kikao hicho cha Kamati Kuu kilichokuwa chini ya Mwenyekiti wake Rais mstaafu, Jakaya Kikwete, kimeteua majina matatu ya wanachama wake waliowania nafasi ya uspika wa Bunge.

Nape aliwataja walioteuliwa kuwa ni Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Tulia Akson na Abdullah Ally Mwinyi.

“Kikao hicho cha kamati ya wabunge wote wa CCM kitapiga kura kwa ajili ya kumpata mgombea mmoja,” alisema Nape.

Kamati kuu ilikuwa na kibarua cha kuchambua zaidi ya majina 20 ya makada wake waliochukua fomu za kuwania nafasi ya uspika wa Bunge.

Wanachama waliochukua fomu kuwania nafasi hiyo ni pamoja na aliyekuwa Spika wa Bunge la tisa, Samuel Sitta, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Dk. Emmanuel Nchimbi, aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Costa Mahalu, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum, Ritha Mlaki na aliyekuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam Dk. Didas Massaburi.

Wengine ni Dk. George Nangale, Dk. Medard Kaleman, Julias Powertiller, Agnes Makune, Mwalika Watson, Muzamil Kalokola, Simon Rubugu, Veraikunda Urio, Gosbert Blandes, Banda Sonoko na Leonce Mulenda.

Akizungumzia nafasi ya unaibu spika, Nape alisema kwa mujibu wa kanuni za kamati za wabunge wote wa CCM, Toleo la 4 mgombea wa nafasi hiyo ya maombi na kuiwasilisha kwa Katibu wa Kamati ya Wabunge wa CCM.

“Fomu za nafasi ya mgombea wa unaibu spika zitaanza kutolewa kuanzia leo hadi kesho saa 10 jioni na uchaguzi utafanyika kesho hiyo hiyo ili kumpata mgombea wa CCM,” alisema.

Sitta atafakari

Baada ya maamuzi hayo ya kikao cha CCM, MTANZANIA ilimtafuta Sitta ili kujua alivyopokea uamuzi huo wa kikao cha CC, ambapo alisema bado hajaarifiwa kuhusu kuenguliwa kwake katika kinyang’anyiro hicho.

“Mimi sijasikia, siwezi kusema kitu nisichokijua kwa kawaida huwa tunaitwa tunaambiwa kasoro hizi na zile basi. Sijazijua sababu, kama tumetolewa kwa ubaguzi au nimetolewa kwa kuonewa ndiyo maana nasema inabidi tusikilize kwanza,” alisema.

Hivi karibuni katika moja ya vyombo vya habari Sitta alikaririwa akisema kuwa safari hii hatokubali jina lake likikatwa kwa hila kwa kutumia vigezo vya ubabaishaji kama ilivyokuwa mwaka 2010 wakati akiwania nafasi hiyo.

Sitta ambaye ni mbunge mstaafu wa Jimbo la Urambo, alisema na kuonya kuwa endapo kama chama chake kitatumia vigezo ili kuwabeba watu fulani kama ilivyofanyika 2010, atakwenda mahakamani kufungua kesi ya kikatiba kupinga mchakato huo.

Mwanasiasa huyo alikiri kwa kusema kwamba katika mchakato wa urais alikatwa kwa kigezo cha umri mkubwa, huku akionya jambo hilo lisitokee katika kinyang’anyiro cha uspika ndani ya chama chake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles