26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NBS yatakiwa kutoa elimu ya sensa

Na Ramadhan Hassan,Dodoma

OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS), imetakiwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na umuhimu wa kuhesabiwa katika zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika mwakani  ili kuiwezesha Serikali kupanga maendeleo na kukuza uchumi. 

Akichangia leo,Agosti 18,2021,katika  kikao cha uhamasishaji na utoaji wa elimu ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 kwa viongozi wawakilishi wa Serikali  ngazi mbalimbali,makundi ya kijamii na viongozi wa dini, Kiongozi wa Makanisa ya Kipentekoste,Antony Lyashimba ameiomba NBS kujikita zaidi katika utoaji wa elimu kabla ya kuanza kwa zoezi hilo.

Amesema wanaiunga mkono Serikali katika jambo hilo lakini elimu inahitajika zaidi ili watanzania waweze kulijua zoezi hilo kwa kina kabla ya kufika mwaka 2022 ambao ndio zoezi hilo litafanyika.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi,Wilaya ya Bahi,Stewart Masima, amesema kumekuwa na upotoshaji mkubwa katika zoezi la uchomaji wa chanjo ya Corona sababu zikiwa ni watanzania kutokupewa elimu hivyo ameiomba NBS kuhakikisha inatoa elimu kwa kina pamoja na kutoa vipeperushi.

Kwa upande wake,Spika wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Kongwa,Job Ndugai amesema zoezi hilo ni muhimu kwa Taifa kwani litasaidia nchi kupanga maendeleo hivyo watanzania wanatakiwa kujitokeza kwa wingi katika zoezi hilo.

“Tarehe 31 vikao vyetu vya Bunge vitaanza na vikao vilivyopita tumepitisha mambo mengi ikiwemo na tozo,safari hii itakuwa salama.Hili ni jambo muhimu sana hivyo niwaombe watanzania wajitokeze kwa wingi,sisi wagogo hata zoezi la kuhesabu mifugo linakuwa na shida ni utamaduni wetu,”amesema.

Naye,Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Mbunge wa Kibakwe,George Simbachawene amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Antony Mtaka  kwa kuandaa mkutano huo huku akisisitiza kwamba sensa ni muhimu kwani inaleta ushahidi wa kisayansi na maendeleo.

Kwa upande wake,Mtakwimu Mkuu wa Serikali,Dk.Albina Chuwa amesema Serikali imejipanga kikamilifu  kusimamia  zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa  kufanyika mwakani huku akitoa wito kwa watanzania kujitokeza kwa wingi wakati wa zoezi hilo.

“Sensa hii itakuwa ni ya sita itasimamiwa na serikali ya awamu ya sita kwa weledi  mkubwa tunatarajia watahesabiwa zaidi ya watu milioni 64 kwani kila mwaka watu wanaongezeka milioni 3.1 na sensa mwisho ya mwaka 2012 tulikuwa milioni 49,”amesema.

Amesema kwa sasa wanauzoefu wa kutosha na wamejipanga kuhesabu watu mbalimbali ikiwemo watu wenye ulemavu ambapo ambapo amedai zoezi hilo lipo kwa mujibu wa sheria hivyo ni lazima watu wahesabiwe.

Naye,Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Anthony Mtaka amesema wameandaa kikao hicho na kuyashirikisha makundi yote lengo likiwa ni kuhamasishaji na utoaji wa elimu ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles