31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

NATAMANI  JPM UKISTAAFU UONJE  TUZO YA MO IBRAHIM

TUZO yenye thamani ya Dola za Marekani  milioni 5, hutolewa kila mwaka kwa Rais wa nchi ya Afrika aliyeboresha usalama, afya, elimu, maendeleo ya kiuchumi na haki za kisiasa katika nchi yake na kukabidhi madaraka kwa misingi ya kidemokrasia kwa mrithi wake.

Kwa mara nyingine, wakfu wa Mo Ibrahim, Jumanne ya Machi  28, mwaka huu,  ulitangaza kuwa hajapatikana kiongozi  ambaye amekidhi sifa zote zinazohitajika katika mwaka 2016, ikiwa ni  mara ya sita katika miaka kumi tangu kuanzishwa tuzo hiyo mwaka 2006.

Ni Marais wa zamani watano tu kutoka Afrika ndio walishapata tuzo hii,  huku  mara ya mwisho tuzo hiyo akiwa  amepewa  Rais wa zamani wa Namibia Hifikepunye Pohamba, mwaka 2014.

Wengine waliowahi kuipata ni Pedro Pires wa Cape Verde, Festus Mogae  wa Botswana, Joachim Chissano wa Msumbiji na Nelson Mandela wa Afrika Kusini.
 

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa tuzo hiyo, Dk. Salim Ahmed Salim wakati  akitoa tangazo la kutompata mshindi alisema kuwa,  tuzo hiyo ina vigezo vya juu kama  vilivyoorodheshwa  katika haya ya kwanza  na vinawalenga viongozi ambao kabla ya kustaafu waliyaongoza mataifa yao vizuri, jambo ambalo si kawaida Afrika.

Hakika vigezo hivi vimeendelea  kuwabwaga hata viongozi wetu wa Tanzania  ambao kwa miaka mingi tangu kupata uhuru wamekuwa wakijinadi kuwa wanaongoza kwa kufuata misingi ya Sheria na Utawala Bora.

Rais John Magufuli unayo sababu ya   kuibuka kidedea kwa kuitwaa  tuzo hii kwa  mara ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki,  endapo utazingatia vigezo husika.

Kiusalama, majeshi yetu yamejitahidi  kwani mipaka  iko salama na vitendo vya ujambazi vimepungua. Lakini Je, vipi  migogoro  kati ya wakulima na wafugaji? Je, watu wanaojichukulia sheria mikononi?  Je , ukatili dhidi ya watoto na wenye ulemavu wa ngozi?

Kwa upande wa afya Serikali inajitahidi lakini jambo la kujiuliza ni Je, watu wenye kipato duni  hawawezi  kupoteza maisha  kwa  kushindwa kugharimia matibabu? Je, hospitali  za Serikali zina  dawa za uhakika?   Je, maeneo ya vijijini vituo  vya afya vinatosha?             

Elimu inapewa  kipaumbele na Serikali kwani kuanzia chekechea  mpaka kidato cha nne hakuna kulipa ada. Lakini  hizi shule za Serikali zina sifa ya kumfanya mhitimu kujitambua? Na kama ni ndiyo, mbona wananchi wengi wakiwamo watawala hupenda  kupeleka watoto wao shule binafsi?

Maendeleo ya  kiuchumi kwa mantiki ya viwanda  kuna safari ya  matumaini, lakini Je, vipi  wakulima huko vijijini ambao wengi wao  hutegemea  matrekta ya kutumia damu tena bila msaada wa uhakika wa maafisa ugani, miundombinu  ya umwagiliaji  huku  wakihimizwa kulima ili wasife  njaa hata kama kuna  ukame wa muda mrefu?

Je, viongozi wa vyama vya siasa pamoja na wafuasi wao wanapewa haki zao za kisiasa kama vile  kukusanyika? Je, waandishi wa habari na vyombo vya habari ni sauti ya wasio na sauti?

Kwa muda mrefu Serikali yetu ya Muungano imekuwa na utamaduni  mzuri  wa  viongozi  kukabidhiana madaraka japo ni ndani ya CCM tu, lakini Je, kwa upande wa Zanzibar ambapo pameendelea kuwapo manung’uniko kwamba kuna hujuma za kisiasa haliwezi kuwa doa?

Wafaransa wana msemo usemao: ‘‘Vouloir c’est Pouvoir’’ tafsiri yake ikiwa ‘‘Kutaka ni Kuweza.’’ Naamini Rais wetu mpendwa Magufuli ukitaka utaweza na hatimaye baada ya kustaafu utaibeba  tuzo ya MO IBRAHIM.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles