27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

NASA, JUBILEE WATUHUMIANA UKABILA, UPENDELEO

NAIROBI, KENYA

SHUTUMA kati ya vyama vya Jubilee na National Super Alliance (NASA) kuhusu mrengo upi unaendeleza zaidi ukabila na upendeleo wa kidugu, unazidi kuibua mjadala mkali nchini hapa.

Mvutano huo ulitokana na hatua ya Chama cha Wiper kumteua mtoto wa kiongozi wake, Kalonzo Musyoka kuwa mbunge katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA).

Kiongozi wa Wengi Bungeni, Aden Duale aliapa kupinga kabisa kuteuliwa kwa wakili huyo mchanga, Kennedy Kalonzo, akisema Jubilee haitaruhusu viongozi wa upinzani kuteua watu wa familia zao katika nyadhifa za kitaifa.

Muda mfupi baada ya matamshi ya Duale, Naibu Rais William Ruto alisema kuwa sasa upinzani hauna misingi yoyote ya kimaadili kuikosoa Jubilee kuhusu ukabila na upendeleo wa kidugu.

“Wamekuwa wakituambia kuwa hawataki ukabila, lakini wamewateua watoto na ndugu zao kwa nyadhifa za EALA,” alisema akirejea uteuzi wa kijana wa Musyoka na ndugu mkubwa wa mgombea urais wa Nasa, Raila Odinga, Dk. Oburu Oginga.

Hata hivyo, Oginga alifuatilia mbali uamuzi wa kumteua siku tano zilizopita.

Lakini pia imethibitika kupitia vyanzo vya habari vya uhakika katika wizara ya mambo ya nje ya Kenya kuwa binti wa naibu rais, June Chepchirchir, anashikilia wadhifa wa juu wa kansela wa pili katika ubalozi wa Kenya mjini Rome, Italia.

Ingawa amehitimu katika masuala ya kimataifa na diplomasia, duru hizo zilisema alifikia wadhifa huo wa juu kwa haraka isivyo kawaida.

Mmoja wa viongozi wakuu wa Nasa na waziri wa zamani wa mambo ya nje, Moses Wetangula, alionekana kuashiria jambo hilo alipoishutumu Serikali ya Jubilee kwa kuteua kiholela watoto na jamaa za Rais Uhuru Kenyatta na naibu rais katika balozi pasipo sababu zozote za ujuzi isipokuwa uhusiano wa kifamilia.

Katika matamshi yake kumjibu naibu rais, Wetangula alitoa mfano wa wapwa wa Kenyatta, Jomo Gecaga, anayehudumu Ikulu kama katibu binafsi wa rais na Nana Gecaga anayehudumu kama Meneja Mkurugenzi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Kenyatta (KICC).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles