24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

NAPE, MBOWE WAONGOZA WAOMBEZAJI MSIBA WA MPOKI

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Moses Nnauye, akitoa heshima za mwisho kwa marehemu Mpoki Bukuku,mpiga picha wa Gazeti la The Guardian, katika eneo la uwanja wa Shule ya Wazazi, Tabata Kimanga jijini Dar es Salaam jana.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Moses Nnauye, akitoa heshima za mwisho kwa marehemu Mpoki Bukuku,mpiga picha wa Gazeti la The Guardian, katika eneo la uwanja wa Shule ya Wazazi, Tabata Kimanga jijini Dar es Salaam jana.

Na TUNU NASSOR,-DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasi na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, jana waliongoza mamia ya waombelezaji kuaga mwili wa aliyekuwa Mpigapicha na mwandishi wa magazeti ya The Guardian Limited, marehemu Mpoki Bukuku (44).

Shughuli hiyo ya kuaga mwili wa marehemu Bukuku, zilifanyika katika Uwanja wa Shule ya Sekondari ya Wazazi Tabata jijini Dar es Salaam ambapo wawakilishi kutoka makundi mbalimbali walitoa salamu zao za rambirambi kwa familia ya marehemu pamoja na wana tasnia ya habari nchini.

Mpoki alifariki Ijumaa katika Taasisi ya mifupa (MOI) alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu baada ya kugongwa na gari eneo la Mwenge ITV jijini Dar es Salaam.

Akitoa salamu kwa familia ya marehemu, Waziri Nape, alisema kuwa tasnia ya habari imepoteza mtu muhimu aliyetumia taaluma yake kutoa mchango mkubwa kwa Taifa.

Kutokana na msiba huo Nape, aliwataka wanahabari nchini kuiga mfano wa marehemu Bukuku  ambaye alifanyakazi nzuri na kubwa enzi ya uhai wake.

Kwa upande wake Mbowe, alimwelezea Bukuku kama mpambanaji na aliyefanya kazi zake kwa weledi mkubwa.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile alitumia fursa hiyo kumwomba Waziri Nape kufikisha ujumbe serikalini ikiwemo kwa wakuu wa wilaya kutowaona waandishi wa habari kama maadui wa Serikali.

“Mheshimiwa Waziri Nape leo (jana) tunamwaga mwenzetu hapa Mpoki Bukuku na ni wazi kila mmoja amezungumza namna alivyofanyakazi zake kwa weledi. Ila kwangu tunakuomba tufikishie salamu serikali maana kuwa waandishi wa habari si maadui wa Serikali.

“Sasa wakiripoti habari ya njaa siku ya pili chakula kinapelekwa mwandishi anakamatwa na kuwekwa ndani kwa uchochezi.

“Lakini si hilo tu sasa imefika wakati waandishi wanapigishwa magoti na wakuu wa wilaya, ninakuomba ufikishe kilio chetu kwa serikali kuwa waandishi wa habari si magunia ya kujifunzia kazi,” alisema Balile.

Mbali na viongozi hao wengine waliohudhuria ni pamoja na Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu pamoja na wawakilishi kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi.

Mwili wa marehemu ulisafirishwa jana kwenda Dodoma kwa mazishi yatakayofanyika leo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles