33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NAIBU JAJI MKUU KENYA AKAMATWA KWA RUSHWA

NAIROBI, KENYA


NAIBU Jaji Mkuu wa Kenya, Philomena Mwilu amekamatwa katika Mahakama ya Juu mjini hapa kwa tuhuma za rushwa.

Baada ya kukamatwa jana, Jaji Mwilu alichukuliwa na Kurugenzi ya Uchunguzi wa Makosa ya Jinai   kuhojiwa tuhuma zinazomkabili.

Muda mfupi baada ya kukamatwa kwake, Mkurugenzi wa Mashitaka ya Umma (DPP), Noordin Haji akizungumza na    waandishi wa habari kueleza suala hilo.

Haji alisema ofisi yake ina ushahidi wa kutosha kumshitaki Jaji Mwilu mahakamani.

DPP alisema Jaji Mwilu atashitakiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka, kupokea rushwa na kushindwa kulipa kodi.

Haji alisema alikuwa Mahakama ya Juu kumfahamisha Jaji Mwilu juu ya mashitaka yanayomkabili.

Kukamatwa kwake kunafuatia mlolongo wa mikutano ya Tume ya Utumishi ya Ujaji (JSC), ambayo ni mwajiri wa wafanyakazi wa mahakama, kwa sehemu kubwa ya asubuhi jana.

Kinachovutia zaidi Jaji Mwilu pia alihudhuria mikutano hiyo na haikuweza kufahamika mara moja iwapo anashughulikiwa na mwajiri wake.

Haji na Ofisa Mwandamizi wa Kupambana na Jinai, George Kinoti walihudhuria baadhi ya mikutano kabla ya Jaji Mwilu kukamatwa.

Wafanyakazi wa Mahakama ya Juu waliendelea na shughuli zao kama kawaida, lakini wengi wao wakikwepa kuonana na waandishi wa habari.

Kukamatwa kwa ofisa wa juu katika idara ya mahakama si kitu cha kawaida katika historia ya Kenya na ni matokeo ya uchunguzi wa wiki kadhaa juu ya kukithiri rushwa katika mfumo wa mahakama na tukio hilo linatarajia kuitikisa taasisi hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa, Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA) ilimripoti Jaji Mwilu kwa Haji baada ya kubainika miamala mikubwa ya fedha inayoingia na kutoka katika akaunti zake za benki.

Awali uchunguzi ulikuwa ukipitia miamala ya fedha iliyochangia anguko la Benki ya Imperial na kushindwa kwake kulipa kodi serikalini.

Katika uchunguzi huo pia ikabainika Jaji Mwilu alikiuka sheria ya uongozi na maadili kwa kukubali mkopo binafsi wa Sh milioni 12 za Kenya (Sh milioni 250 za Tanzania) kutoka Benki ya Imperial.

Jaji Mkuu David Maraga, ambaye anaiongoza taasisi hiyo ya mahakama, aliwahi kusema hakuna ‘ng’ombe mtakatifu’ hata katika   mahakama linapokuja suala la kupambana na rushwa.

“Sina muda na maofisa wa mahakama wala rushwa. Fahamu uko peke yako na usitarajie huruma au ulinzi kutoka ofisi yangu,” Jaji Maraga aliwahi kuwaonya maofisa wa mahakama Juni mwaka huu.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles