23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

NACTE YAFUTA USAJILI WA VYUO 20

 

na aziza masoud- dar es salaam

WAKATI udahili wa wanafunzi wa vyuo ukianza jana Baraza la Elimu na Mafunzo ya Ufundi (Nacte), limefuta usajili wa vyuo 20 kwa kushindwa kufuata taratibu zinazoendana na matakwa ya usajili.

Miongoni mwa vilivyofutwa vipo vyuo viwili maarufu vya Dar es Salaam ambavyo ni Chuo cha Uandishi wa Habari cha Royal College of Tanzania na Techno Brain.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Kaimu Katibu Mtendaji wa Nacte, Dk. Adolf Rutayuga, alisema kufungwa kwa vyuo hivyo ni matokeo ya ukaguzi uliofanyika kuanzia Julai hadi Septemba, mwaka jana uliohusisha vyuo 458.

Alisema kati ya vyuo hivyo vilivyokuwa vimesajiliwa, 426 vilikutwa na vigezo vya kutoa mafunzo wakati 32 vilikutwa na kasoro.

“Baraza limeamua kufuta usajili wa vyuo 20 kati ya 32 vyenye kasoro, hatua hii imekuja baada ya wahusika kushindwa kufuata taratibu zinazoendana na matakwa ya usajili wa vyuo hivyo, uamuzi huu umefikiwa kwa kuzingatia kifungu cha 20 cha Kanuni za Usajili wa Vyuo vya Ufundi cha mwaka 2001,” alisema Dk. Rutayuga.

Alitaja vyuo vingine vilivyofutiwa usajili kuwa ni Chuo cha Masomo ya Biashara cha Covenant na Chuo cha Ufundi cha Mugerezi Spatial vyote vipo Dar es Salaam.

Vyuo vingine vilivyofutiwa usajili vilivyopo Dar es Salaam ni Chuo cha Biashara cha Lisbon, Chuo cha Mafunzo cha PCTL na Chuo cha Sayansi ya Tiba cha St. Peters.

Alisema vyuo vingine ni Chuo cha Mafunzo ya Biashara na Utawala cha Dacico, Chuo cha Ustawi wa Jamii kilichopo Mbeya na Chuo cha Utalii Musoma ambacho kipo Shinyanga.

Dk. Rutayuga alitaja sababu ya kufutiwa usajili kwa vyuo hivyo na katika orodha hiyo pia vimo vikongwe ni pamoja na kutokujitosheleza kwa miundombinu ya kujifunzia katika vyuo hivyo.

“Vyuo vyote vinaposajiliwa kunakuwa na makubaliano ya kuendelea kuboresha  baadhi ya vitu ikiwemo miundombinu ya majengo, vifaa vya kujifunzia na kufundishia na walimu wahusika wasipotekeleza hilo kwa muda unaotakiwa wanakuwa hawajakidhi vigezo vya kuendelea kuwa na usajili,” alisema.

Dk. Rutayuga alisema tayari wameshaviandikia barua vyuo hivyo kuhakikisha vinawahamisha wanafunzi waliopo katika vyuo vingine vinavyotoa programu zinazoendana na walizokuwa wakizitoa.

Pia alitaja vyuo tisa vilivyozuiliwa kudahili wanafunzi wapya kwa mwaka wa masomo wa 2018/2019 kwa kuzingatia kifungu cha 22 (1) cha kanuni za usajili wa vyuo vya ufundi cha mwaka 2001.

Alitaja vyuo hivyo kuwa ni Chuo cha Biashara cha Montfort, Chuo cha Mazingira na Maendeleo Endelevu, Chuo cha Biashara na Utawala cha Silva, Chuo cha Biashara na Uwekezaji Tanzania vyote vipo Dar es Salaam.

“Vyuo hivi vimezuiliwa kusajili kwa mwaka huu wa masomo, hata hivyo wanafunzi waliopo katika vyuo hivyo wanaruhusiwa kuendelea na masomo kama kawaida hadi watakapohitimu mafunzo yao,” alisema.

Pia alisema wamesitisha programu za mafunzo zilizokuwa zikiendeshwa bila kuidhinishwa katika vyuo vitatu vya utabibu nchini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles