24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

‘Nacte simamieni Tanzania ya Viwanda’

NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo
NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo

NA MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk. Leonard Akwilapo, amesema Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) lina dhamana kubwa ya hatima ya elimu ya ufundi nchini.

Amesema ili kufikia kutimiza suala hilo kuelekea kwenye uchumi wa Tanzania ya viwanda, ni lazima baraza hilo lijenge misingi imara kwa kuhakikisha wanatoa elimu na kufanya ukaguzi kila wakati.

Kauli hiyo aliitoa jana jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na watendaji wa baraza hilo katika uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi ambapo alisema agenda hiyo inabidi ichukuliwe  kama kigezo cha kupima utendaji wa kazi wa Nacte.

“Ni matumaini yangu kuwa wajumbe wote wa baraza hili tunalolizindua leo watatambua hili na kutoa mchango maridhawa katika maendeleo ya taifa na kufanikisha agenda ya Taifa la Uchumi wa Viwanda,” alisema Dk. Akwilapo.

Alisema uzinduzi wa baraza hilo ulikuwa ni muhimu sana katika historia ya Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE), kwa sababu kama taasisi imekuwa haina Baraza la Wafanyakazi kwa kipindi.

“Natambua kwamba kwa kipindi chote cha uhai wa taasisi tangu ilipoanza shughuli zake takribani miaka 15 iliyopita, mmekuwa mkiendesha shughuli zenu bila kuwa na chombo hiki. Na hiyo ni kinyume kabisa na taratibu za utawala bora.

“Sina budi kuwapongeza kwa kutambua hilo na kuamua sasa kuanza kutekeleza majukumu yenu kulingana taratibu,” alisema.

Naibu katibu mkuu huyo alisema alifahamu kuwa nia na juhudi za kutaka kuunda Baraza la Wafanyakazi la taasisi hiyo zilianza muda mrefu yapata miaka nane iliyopita.

“Utaratibu wa kuundwa kwa Baraza la Wafanyakazi unahitaji kuwepo na makubaliano ya pande mbili, upande wa mwajiri kwa upande mmoja na Chama cha Wafanyakazi mahali pa kazi kwa upande mwingine. Kwa sasa hali ni tofauti kwa kuwa ‘TUGHE’ moja ya chama cha wafanyakazi nchini kimefanikiwa kuanzisha tawi lake hapa na hatimaye kuwezesha kuundwa kwa baraza hili la wafanyakazi,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi wa Nacte, Mhandisi Stephen Mlote,  alitaja majukumu ya Baraza la Wafanyakazi kuwa ni pamoja na kuwashirikisha wafanyakazi wa Nacte katika utekelezaji wa shughuli za Nacte kwa kushirikiana na uongozi.

Majukumu mengine ni kushauri Nacte  juu ya ufanisi wa kazi na hatua zinazofaa kuchukuliwa na kuhakikisha kuwa huduma zitolewazo na Nacte ni za kuridhisha na zimo katika lengo la kujenga taifa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles