27 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Mwarobaini kwa wakopaji benki wasiorejesha fedha wapatikana

Na SHEILA KATIKULA

MWANZA

WATU waliokuwa na mazoea ya kukopa fedha benki tofauti kwa wakati mmoja na bila kukamilisha marejesho yote, sasa wamewekewa kibano baada ya Taasisi ya Dun & Bradstreet Credit Bureau Tanzania Ltd kupewa jukumu la kuwadhibiti.

Kauli hiyo ilitolewa jijini hapa jana na Meneja Biashara na Maendeleo wa Dun & Bradstreet, Josephine Temu, katika semina kwa wafanyabiashara, vikundi vya saccos na mameneja wa benki mbalimbali.

 “Ili kuweza kukopesheka kwa urahisi ni vema kujua deni lako katika benki fulani  kabla ya kukopa sehemu nyingine, tukizingatia hayo tutalinda taasisi zinazotoa mikopo ili zisiweze kufilisika.

 “Tumekuja na mpango huu wa ufuatiliaji wakopaji na tumefanya maboresho ili ukikopa benki fulani uonekane benki nyingine, awali watu walikuwa wakichukua mikopo katika taasisi moja na kwenda kwingine tena bila kujulikana, lakini sasa watajulikana.

 “Kibaya zaidi wakopaji wa namna hiyo walikuwa wanazifanya benki kutokuwa salama, lakini hivi sasa hautakopa sehemu tofauti bila kujulikana, pia kuna watu walikuwa hawajui kama taarifa zao za mikopo zilikuwa zitatunzwa,” alisema.

Alisema hivi sasa taasisi yoyote iliyojisajili kupitia kampuni hiyo inaweza kuzipata taarifa za mkopaji na kufanya tathimini ili kuona kama mteja anaweza kukopesheka ama hakopesheki.

Kwa upande wake, Meneja Msaidizi Kitengo cha Ubadilishaji wa Taarifa za Ukopaji kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Mkanwa Magina, alisema mbali na kuwa na mfumo wa utunzaji wa kumbukumbu za mkopaji, lakini pia ni muhimu kutambua mienendo ya wakopaji.

Magina alisema katika kuhakikisha hilo linafanikiwa, taasisi hiyo imepewa jukumu la kuchakata taarifa za wakapoji na aliwataka wananchi na wakopaji wakawa na taratibu za kufuatilia taarifa zao kwa sababu zina faida kwao.

Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Vanson Microfinance, Higini Mwacha, alipongeza uwepo wa mfumo huo kwa sababu unakusudia kuondoa changamoto na taarifa zisizo za kweli kutoka kwa wakopaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles