25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mwanasheria: Janga la ubaguzi’ lilisababisha kifo cha George Floyd

MINNEAPOLIS, MAREKANI

MWANASHERIA wa George Floyd amewaambia waandishi wa habari kuwa janga la ubaguzi limesababisha kifo chake.

Watu waliokusanyika kutoa heshima zao siku ya Alhamisi walikaa kimya kwa dakika nane, sekunde 46, muda ambao Floyd anadaiwa kuwa chini mikononi mwa polisi mjini Minneapolis.

Mamia walihudhuria tukio hilo, ambalo pia mwanaharakati wa asasi za kiraia Mchungaji Al Sharpton alitoa ujumbe wake akisema ni muda sasa wa kusimama; ” ondoa mguu wako kwenye shingo zetu”, alisema.

Mauaji ya Floyd, yaliyopigwa picha ya video, yamesababisha ghadhabu na wimbi la maandamano katika miji mbalimbali nchini Marekani.

Wakati huohuo, maofisa polisi watatu wameshtakiwa kwa makosa ya kusaidia mauaji ya Floyd  na wamefikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza . 

Dhamana ya dola milioni moja iliwekwa lakini itapunguzwa hadi dola 750,000 ikiwa watasalimisha silaha zozote wanazomiliki na kutimiza masharti mengine, alisema jaji wa mahakama.

Derek Chauvin, ofisa aliyeendelea kuikaba shingo ya Floyd kwa mguu wake wakati akilalama kuwa hawezi kupumua, ameshutumiwa kwa mauaji ya kiwango cha pili na anatarajiwa kufikishwa mahakamani siku ya Jumatatu.

Maandamano kwa siku nane zilizopita yamekuwa ya amani lakini baadhi wamejiingiza katika vitendo vya vurugu, huku muda wa kukaa nje ukiwekwa katika miji kadhaa nchini Marekani.

Akizungumza katika kusanyiko la kutoa heshima kwa Floyd, wakili Benjamin Crump amesema si ”janga la corona lililomuua Floyd ni janga la ubaguzi wa rangi limemuua Floyd.”

Wakili huyo alisema kifo cha Floyd kilipangwa

Familia ya Floyd, Gavana wa Minnesota Tim Walz, Seneta wa Minnesota Amy Klobuchar na Meya wa Minneapolis Jacob Frey ni miongoni mwa mwa watu waliofika katika tukio la heshima kwa Floyd katika Chuo Kikuu cha North Central mjini Minneapolis.

Mmoja wa ndugu wa Floyd, Philonise Floyd ameeleza namna familia ilivyokuwa masikini na namna walivyokuwa wadogo na George alikuwa akifua nguo kwenye bomba na kuzikausha kwa mashine ya kupashia moto chakula.

”Watu wote hawa wamekuja kumuona kaka yangu, inashangaza aligusa mioyo ya watu wengi sana,” alisema.

Mchungaji Al Sharpton pia ametaka waliohusika katika tukio hilo kwa namna moja ama nyingine kuwajibika.

”Hatutaacha, alisema , akimaanisha maandamano ambayo yameshika kasi katika majimbo mbalimbali nchini humo. ”Tutaendelea hadi tutakapobadili mfumo wa haki.”

Wakati huo huo aliyekuwa Waziri wa Ulinzi wa Marekani James Mattis amemshutumu Rais Donald Trump, kwa kuleta mgawanyiko na kutumia vibaya mamlaka yake.

Katika maoni aliyotoa jambo ambalo si la kawaida, Mattis alisema rais ameamua kugawanya watu wa Marekani na pia ameshindwa kuonesha uongozi uliokomaa.

Anasema alikasirishwa na kufadhaishwa sana na jinsi Trump alivyoshughulikia maandamano ya hivi karibuni.

Mattis alijiuzulu 2018 baada ya rais kuamua kuondoa majeshi ya Marekani kutoka Syria.

Tangu wakati huo amekuwa kimya hadi utawala wa Trump ulipokosolewa vikali katika gazeti la Atlanta Jumatano.

Kama jibu lake kuhusu ukosoaji huo, Trump alituma mfululizo wa ujumbe kwenye Twitter ambapo alisema Mattis alisemekana kuwa ofisa wa thamani ya juu zaidi duniani.

“Sikupenda mtindo wake wa uongozi au yeye mwenyewe na wengine wengi wanakubaliana na hilo, “Afadhali aliandika!”

“Donald Trump ndio rais wa kwanza kwa maisha yangu ambaye hawaunganishi raia wa Marekani – hata hajifanyi pengine anajitahidi katika hilo,” Mattis aliandika katika gazeti la The Atlantic. “Badala yake, anajitahidi kutugawanya.”

Aliendelea kusema kuwa : “Tunashuhudia miaka mitatu ya hatua hizi za kukusudiwa. Tunashuhudia matokeo ya miaka mitatu ya uongozi ambao haujakomaa.

Mattis pia alizungumzia wimbi la hivi sasa la maandamano dhidi ya ubaguzi wa rangi yaliyochochewa na kifo Floyd.

‘Nimechoka kuogopa’: Ni kwanini Wamarekani wanaandamana? maandamano haya yanafafanuliwa na dhamira ya maelfu ya watu ambao wanasisitiza kwamba tuishi kulingana na maadili yetu… kama taifa,” Mattis aliandika. 

“Hatustahili kutatizwa na wachache ambao ni wavunjaji wa sheria.”

Ofisa huyo aliyestaafu – ambaye alijiuzulu Desemba 2018 alikosoa vikali sera ya kigeni ya rais – na pia akashtumu utumiaji wa jeshi kama njia ya kujibu maandamano yanayotokea.

“Sikuwahi kufikiria kwamba jeshi… litaamrishwa kwa chochote kile kitakachotokea kukiuka haki ya kikatiba kwa raia wake wenyewe,” alisema.

“Kufanya wanajeshi kama njia ya kutatua hili, kama ilivyoshuhudiwa Washington DC, kunasababusha mgogoro… kati ya jeshi na raia,” aliongeza.

Mashtaka hayo yanamaanisha nini?

Mauaji ya kiwango cha kwanza na pili chini ya sheria ya Minnesota yanahitaji ushahidi kwamba mshtakiwa alikusudia kuua. 

Shitaka la mauaji kiwango cha kwanza katika kesi nyingi kunahitajika ushahidi kuonesha alikusudia kuua na mauaji kiwango cha pili yanahusiana kwa karibu uhalifu uliodhamiriwa.

Shitaka la mauaji kiwango cha tatu kutahitaji ushahidi kwamba mshtakiwa alitaka mwathirika kufa ila tu vitendo vyake vilikuwa hatari mno na vilitekelezwa bila kuzingatia ubinadamu.

Katika mauaji ya kiwango cha pili, mtu akipatikana na hatia anaweza kufungwa hata miaka 40, miaka 15 zaidi ya shtaka ya mauaji kiwango cha tatu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles