30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mwanamke akutwa juu ya paa Wizara ya Fedha

Mwanamke akutwa juu ya paa Wizara ya FedhaNA JONAS MUSHI, DAR ES SALAAM

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, mwanamke mmoja amepanda katika paa la jengo la Wizara ya Fedha na Mipango huku tukio hilo likizua sintofahamu kwa wafanyakazi wa wizara hiyo na wapita njia.

Tukio hilo lilitokea jana Dar es Salaam majira ya asubuhi ambapo mwanamke huyo anayedaiwa kuwa raia wa Kenya alipanda juu ya paa hilo na kuanza kupiga kelele.

Katika tukio hilo ambalo MTANZANIA ilishuhudia, inadaiwa mwanamke huyo aliwasili katika eneo hilo la wizara akionekana kama mmoja wa wananchi ambao walikwenda kwa ajili ya kupatiwa huduma, lakini baada ya muda alionekana akiwa juu ya paa huku akipiga kelele.

Mwanamke huyo aliyekuwa amebeba mkoba, ambaye haikufahamika mara moja nia yake ya kupanda juu ya paa hilo, ilimchukua saa kadhaa akiwa juu na pale walinzi wanaolinda ofisi za wizara hiyo walipokwenda katika eneo hilo na kumwomba ateremke aligoma.

Hata hivyo hali hiyo ilionekana kutowakatisha tamaa walinzi hao wanaolinda majengo ya Wizara ya Fedha na Mipango yaliyopo mita chache kutoka Ikulu ya Dar e Salaam, ambao walikwenda tena wakiwa na ngazi na kuanza kumbembeleza ambapo jaribio hilo lilifanikiwa na mwanamke huyo kuteremka.

Wakati mwanamke huyo akiwa juu ya paa, wananchi waliokuwa chini walianza kumuuliza maswali, lakini hakusikika majibu yake kutokana na kelele za watu ambao kila mmoja aliimuuliza swali lake.

Hata hivyo mmoja wa askari wa kikosi cha Usalama Barabarani ambaye alisogea kwa karibu kumuuliza mwanamke huyo, alisema kuwa alimwambia amechukua uamuzi huo kutokana na kuteswa na askari nchini Kenya.

“Tukio hili ni la ajabu na linaibua maswali… hivi inakuwaje kwa jengo kama hili la wizara ambalo lipo jirani na Ikulu mtu anapanda juu na walinzi wapo?

“Hii inasikitisha sana na ni ajabu kwa kweli, ipo siku tutakuta watu wanaingia Ikulu na kufanya mambo ya ajabu kwa viongozi wetu,” alisema mmoja wa wananchi waliokuwa katika eneo hilo ambaye hakupenda kutajwa jina lake gazetini.

MTANZANIA ilipomtafuta Msemaji wa wizara hiyo, Ingiahedi Mduma ili kuzungumzia suala hilo, alisema kwa sasa yupo mjini Dodoma katika maandalizi ya vikao vya Bunge na hana taarifa ya tukio hilo.

Alipotafutwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Ilala, Lucas Mkondia, alisema hajapata taarifa hizo na kwamba atafuatilia tukio hilo.

“Hatujapata taarifa hizo, ndiyo kwanza nasikia kutoka kwako, labda tufuatilie,” alisema Kamanda Mkondia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles