Na BENJAMIN MASESE – SENGEREMA
MWANAFUNZI wa darasa la saba Shule ya Msingi Mwangika, Mboni Mahano (13) amefariki dunia akiwa anapatiwa matibabu Kituo cha Afya Mwangika, baada ya kula chakula kinachodaiwa kuwa na sumu kwenye sherehe.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro alisema mwanafunzi huyo anadaiwa kula chakula cha sumu wakati wa sherehe iliyofanyika Agosti 22, mwaka huu kwa Dorica Omajigo.
Muliro alisema Agosti 23, mwaka huu, baadhi ya wanawake waliokuwa na watoto walirejea kwa Omajigo kusafisha vyombo na kula chakula kingine kilichokuwa kimebaki, baada ya saa kadhaa walianza kulalamika kuumwa tumbo na kukimbizwa Kituo cha Afya Mwangika, lakini mwanafunzi huyo alifariki dunia akiwa anapatiwa matibabu.
“Walioanza kulalamika ni watu wazima wanne, watoto 14 wote walikimbizwa hospitalini na kulazwa, mpaka sasa wanaendelea kupatiwa matibabu, mwili wa marehemu umehifadhiwa hapo na Jeshi la Polisi linaendelea kufanya uchunguzi.
“Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linafuatilia kwa karibu tukio hili, halitasita kuchukua hatua kali za kisheria kwa yeyote atakayebainika kuhusika na kitendo hiki cha kuweka sumu kwenye chakula,” alisema Muliro.