27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Muleba yapata ufadhili mnono wa huduma za Afya

Na Renatha Kipaka, Muleba

Halmashauri ya Wilaya ya Muleba imesaini mkataba wa miaka mitano wenye thamani ya sh 1.5 bilioni wa ufadhili wa kutoa huduma za afya katika visiwa vya Goziba, Bumbile na Ikuza.

Mkataba huo umesainiwa leo Oktoba 5, 2021 kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Geita ambapo wafadhili ni Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) na The Vine Trust ya Uingereza ambapo Kanisa la AIC ndilo limefanikisha kupatikana kwa wafadhili na meli MV Jubilee Hope itakayokuwa inatumika kutoa huduma.

Katika mkataba huo, mgodi wa dhahabu wa Geita utatoa dola 120,000 kila mwaka kwa miaka 5, shirika la The Vine Trust wametoa meli, halmashauri ya Wilaya ya Muleba itachangia wataalam na dawa huku baadhi ya wataalam watatoka kanisa la AIC na Shirika la The Vine Trust.

Akizungumza wakati wa utiaji wa saini wa mkataba huo, Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Toba Nguvila amewahakikishia usalama watumishi watakaokuwa ndani ya meli pamoja na meli yenyewe.

Amesema kuwa kila mwaka watu takribani 100 wanafariki kutokana na mitumbwi na boti kuzama hivyo meli hii italeta ukombozi mkubwa katika kupunguza vifo vya mama na mtoto.

Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Magongo Justus amewashukuru wafadhili na kuwaomba kuendelea kuisaidia Muleba kutokana na mahitaji kuwa makubwa kwani visiwa viko zaidi ya 25.

Naye Dk. Uzia Mohamed, daktari kiongozi wa mradi wa MV Jubilee Hope, ameeleza kuwa watu wanaoishi visiwani wanakabiliwa na magonjwa kama utapiamlo, kichocho, amiba, malaria na kipindupindu kutokana na kutokuwa na huduma za afya na uelewa juu ya elimu ya magonjwa hayo.

Meli ya MV Jubilee Hope ilianza kutoa huduma tangu mwaka 2014 ambapo kwa mwaka inafanya mizunguko 13 na kila inapokwenda inakaa kwa wiki mbili visiwani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles