24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

MUGABE KUPOKONYWA MASHAMBA 20

HARARE, ZIMBABWE


RAIS wa zamani wa Zimbabwe, Robert Mugabe, anatarajia kunyang’anywa mashamba 20, ambayo aliyapata wakati alipowaongoza maveterani wa vita kuvamia mali za walowezi wa kizungu na kujimilikisha.

Lakini sasa maveterani hao katika mazingira ya nadra wameonyesha mshikamano na vyama vya upinzani kuendesha kampeni mpya ya kumpokonya Mugabe mashamba kadhaa anayomiliki ili yagawanywe upya kwa mamilioni ya Wazimbabwe wenye uhitaji.

Msemaji wa Chama cha Taifa cha Maveterani wa Vita vya Ukombozi, Douglas Mahiya, amethibitisha maendeleo hayo mapya akiwa na viongozi wa Chama cha MDC-T na wale wa Zimbabwe Economic Freedom Fighters (EFF).

Walisema wako pamoja katika kampeni ya kumpokonya Mugabe mashamba 20 na kumwachia moja kama inavyosema sera ya Serikali – mtu mmoja shamba moja.

“Tulimpinga Mugabe kwa sababu ya ufisadi wake na tumesema kwa muda mrefu sera ya mtu mmoja shamba moja lazima itekelezwe bila upendeleo.

“Katika hili hatumuungi mkono wala hatumlengi Mugabe binafsi, lakini huu umekuwa wito wetu kwa sauti za juu kuwa ufisadi wake unanuka kwa kuanzia na wingi wa mashamba anayomiliki,” alisema Mahiya.

Mugabe yuko katika wakati mgumu hata kutoka kwa wakuu wa chama tawala cha Zanu-PF tangu alipong’olewa madarakani Novemba 2017.

Hivi karibuni iliropotiwa mashamba anayomiliki mkewe Grace ya Mazowe, ambako pia alijenga nyumba ya kulea yatima, yalivamiwa na wachimbaji wa dhahabu.

Katibu Mkuu wa MDC-T, Douglas Mwonzora, alisema kampeni hiyo wala haimlengi Mugabe pekee bali wamiliki wote wenye mashamba mengi.

“Kuna viongozi wengine waandamizi katika Zanu-PF na Serikali ambao wanamiliki mashamba mengi. Litakuwa jambo baya kumlenga mtu mmoja au familia moja.

“Watu wote wanaomiliki mashamba mengi wahimizwe kurejesha ili wapewe raia wengine wa Zimbabwe wasio na ardhi,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles