Na Nora Damian, Mtanzania Digital
Mufti wa Tanzania, Abubakar Zubeir amesema utamaduni wa kufuturisha waumini wakati wa Mfungo wa Ramadhani una malipo makubwa siyo tu kwa mfungaji bali hata mfuturishaji.
Ameyasema hayo Machi 12,2025 wakati wa hafla ya futari iliyoandaliwa na familia ya Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela na kushirikisha wateja wa benki hiyo, waumini wa Kiislamu, viongozi wa dini na Serikali.
Amesema mwenye kumfuturisha aliyefunga hupata ujira na malipo makubwa sawa na yule aliyefunga bila hata ya kupungua chochote katika ujira na malipo ya aliyefunga.

“Nimpongeze Bwana Nsekela kwa jambo hili kubwa alilolifanya yeye na familia yake na taasisi yake, hili ndilo alilohimiza Mtume, malipo makubwa unayoyapata mojawapo ni kubarikiwa na Mwenyezi Mungu na tunamuomba akujaalie uendelee na moyo huu,” amesema Mufti Zubeir.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, ameipongeza familia hiyo na kusema imetoa sadaka kubwa na kumpongeza Nsekela kwa hafla hiyo.


Kwa upande wake Nsekela amesema futari hiyo ni sehemu ya shukrani ya kumshukuru Mungu kwa mambo mengi anayowatendea.
“Huu ni mwezi wa toba mwezi ambao waislamu kote duniani wanafunga, tunahimizwa upendo na kumcha Mungu siku zote na iftar hii ni sehemu ya shukrani ya kumshukuru Allah kwa mambo mengi anayotutendea,” amesema Nsekela.