28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mudavadi ajitwisha jukumu la kinara wa upinzani

NA ISIJI DOMINIC

WENGI walitarajia Rais Uhuru Kenyatta angepata wakati mgumu kuhudumu muhula wake wa pili kutokana na kile kilichojiri uchaguzi mkuu uliopita. Ni uchaguzi ulioingia kwenye historia baada ya Mahakama ya Juu zaidi kutupilia mbali ushindi wa chama cha Jubilee.

Hata hivyo, Muungano wa upinzani chini ya mwavuli wa NASA ikiongozwa na Raila Odinga, ulisusa kushiriki uchaguzi wa marudio wakitaka marekebisho katika Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Rais Uhuru alishinda kwa zaidi ya asilimia 90 marudio ya uchaguzi na upinzani ukasisitiza kutomtambua kama Rais wa Jamhuri ya Kenya. Mapema mwaka huu, Raila alijia pisha kama Rais wa Wananchi jambo ambalo lilitabiriwa kumpa wakati mgumu Rais Uhuru kutekeleza alichoahidi wakati wa kampeni.

Lakini Machi 9, mwaka huu, Uhuru na Raila walijitokeza hadharani, wakasalimiana nakutangaza kuzika tofauti zilizojiri wakati wa kampeni na kuamua kufanya kazi pamoja kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Ni tukio ambalo liliwaacha wengi kujiuliza kama kweli sasa upinzani upo na nani anayo jukumu la kuimulika serikali kuhakikisha mambo yanaenda vizuri pasipo mwananchi wa kawaida kuumia. Raila amekuwa akiongea lugha moja na Rais Uhuru na hivi karibuni aliteuliwa na Umoja wa Afrika kuwa Balozi anayeshughulikia miundombinu msingi.

Baada ya Raila kubadilisha upepo, mwanasiasa aliyekuwa anapewa nafasi kuwa kinara wa upinzani ni Kalonzo Musyoka ambaye mara mbili aliwahi kuwa mgombea mwenza wa Raila. Kalonzo ambaye pia ni kiongozi wa Chama cha Wiper alishawahi kuwa Makamu wa Rais Kenya.

Lakini wakati wa mazishi ya baba yake mzazi, Kalonzo alisema yeye atakuwa ‘mtu wa mkono’ wa Rais Uhuru na yuko tayari kushirikiana na serikali yake kutekeleza ajenda nne kuu. Siku chache baada ya kauli yake hiyo, serikali ilimrudishia walinzi wake na kisha kumteua Balozi wa Amani Sudan Kusini akichukua nafasi ya aliyekuwa Rais wa Botswana, Festus Mogae.

Kalonzo kufuata nyayo za Raila kushirikiana na Serikali ya Rais Uhuru kuliacha wengi na maswali kama naye kiongozi wa Chama cha ANC, Musalia Mudavadi, ‘ataukana’ upinzani. Kama ilivyo kwa Uhuru na Raila, Mudavadi ni mtoto wa Mwanasiasa Marehemu Moses Mudavadi na alishawishiwa kujiunga kwenye siasa na Rais Mstaafu Daniel arap Moi lengo likiwa ni kuchukua nafasi ya Marehemu baba yake.

Mudavadi ameshawahi kushikilia nyadhifa mbalimbali serikali ni ikiwamo Makamu wa Rais. Baada ya machafuko yaliyotoka na na Uchaguzi Mkuu wa 2007, Mudavadi aliteuliwa kuwa Naibu Waziri Mkuu. Mara kadhaa amekuwa akishawishiwa na wandani wa Rais Uhuru kufanya kazi na serikali ambapo angepewa kazi za kimataifa kama ilivyo kwa Raila na Kalonzo.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa Amani National Congress amesema hana haja na kupewa kazi na lengo lake ni kuimarisha chama chake kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2022 napia kuwa kinara wa upinzani.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Chama cha Amani, Barack Muluka, kuliko kupata kazi kutoka Ikulu, Mudavadi anaona bora afanye kazi na kiongozi wa Chama cha FordKenya, Moses Wetang’ula na Waziri wa Ugatuzi, Eugene Wamalwa kuhakikisha jamiiya Waluhya wanaongea lugha moja 2022.

Mudavadi anasema yeye ndiye aliyebaki kuipiga darubini serikali na pia yeye ndiye sauti mbadala ya wananchi wanaoutazama upinzani kutekeleza shughuli zake ipasavyo.

“Unajua unapojiunga na serikali unakuwa umefungwa. Kuna mambo ambayo yatakuwa hayakufurahishi kwa mfano deni kubwa la taifa, sakata la wakulima wa mahindi na sukari, lakini kwa sababu ni uwa jibikaji wa pamoja, huwezi kuongea kwa uhuru,” alisema.

Mudavadi anasema sio dhambi mtu kuwa mpinzani na haimaanishi wewe sio mzalendo huku akiukumbusha umma kwamba hata Rais Uhuru alikuwa kiongozi wa upinzani baada yakushindwa na Rais Mstaafu Mwai Kibaki 2002.

Anasisitiza inawezekana kuwa ndani ya upinzani bila ya kuhamasisha vurugu na kwamba upinzani Kenya haijakufa ni mapito inayopita akiamini baadaye itaimarika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles