23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Msekwa: Diaspora wangependa kupata haki ya kupiga kura

Tanzânijas Apvienotâs Republikas ârkârtçjâs un pilnvarotâs vçstnieces Doras Mari Mseèu (Dora Mmari Msechu) tikðanâs ar Latvijas Universitâtes rektoru prof. Mârci Auziòu.Na SARAH MOSSI, STOCKHOLM

WIKI iliyopita tuliendelea na mazungumzo na Mkuu wa Utawala katika Ubalozi wa Tanzania nchini Sweden, Jacob Msekwa ambaye aliendelea kufafanua masuala mbalimbali yanayohusiana na Diaspora na mchango wa  ofisi ya ubalozi. Wiki hii Mwandishi wetu SARAH MOSSI anamalizia mahojiano hayo na ofisa huyo. Endelea…

MTANZANIA: Vipi masuala ya kisiasa yanayoendelea kule nyumbani ikiwamo wakati wa uchaguzi, Diaspora wanashiriki vipi?

MSEKWA: Kiutaratibu kwa sheria zetu sisi hatuna huo utaratibu wa watu kupiga kura zikapelekwa nyumbani. Lakini nakumbuka Mizengo Pinda aliyekuwa Waziri Mkuu alisema watafanya utaratibu ifikapo mwaka 2020 watafanya utaratibu Watanzania popote walipo wapige kura.

Nchi nyingi tu wanao utaratibu huo kama vile Msumbiji, Botswana na Angola. Kwa hiyo tusubirie. Na Watanzania wako wengi wangependa wapate haki yao hiyo. Ukisema kuhamasika Watanzania wamehamasika sana kisiasa na wanafuatilia kwa karibu masuala ya kisiasa yanayoendelea huko nyumbani.

Lakini sisi kama ubalozi tunawatreat Watanzania wote kama Watanzania lakini si kwa mrengo wao wa kisiasa. Na sisi tumewaambia Ubalozi si kituo cha polisi unaweza ukaja na kueleza matatizo yako na tukasaidiana kuyatatua na kufahamishana.

MTANZANIA: Huu utaratibu wa kuajiri watu katika ofisi za ubalozi wakitokea nyumbani ilhali miongoni mwa Diaspora wanao ujuzi unatakiwa lakini kuna gharama kubwa katika kuajiri huyo ofisa,kwa upande wenu mnaliangalia vipi?

MSEKWA: Kuna watu wanaitwa local Staff hapa katika ofisi zetu za ubalozi ambao wako sita na katika hao wanne ni Watanzania Diaspora na wawili si Watanzania. Na huu utaratibu wa Local Staff uko katika ofisi mbalimbali za kibalozi. Lakini Serikali ilishatoa maelekezo kwamba pale alipo Mtanzania mwenye sifa za kuajiriwa mpeni.

Na katika kipindi cha miaka kumi tumeajiri watu watano hapa lakini wanne kati yao ni Watanzania. Lakini bado tunasisitiza kwamba pale inapotokea nafasi ya kazi wameomba watu 20 na wako Watanzania wawili basi tunawapa kipaumbele.

Lakini bado zipo kazi nyingine ni lazima zifanywe na sisi watu wa Diplomasia kwa sababu sisi tumetumwa na Serikali tuje kuwakilisha hapa mfano Balozi na Naibu Balozi hawa lazima wawakilishe. Mimi wa upande wa majukumu yangu  hapa ni kucover shughuli za  kidiplomasia na kisiasa.

Kwa hiyo kutoka Tanzania kuja hapa ni sawa na kuhamishiwa idara moja ya Tanzania na kwenda nyingine hapa na sisi ni wapita njia tunakuja na kuondoka.

MTANZANIA: Kuna wanafunzi kutoka Tanzania wanaosoma hapa ofisi ya Ubalozi mnawatambua hawa?

MSEKWA: Moja ya kazi tuliyofanya ni ya kuwaunganisha wanafunzi wa Tanzania kwa sababu ilikuwa tukikutana nao ulikuwa ukiona ni kama vile kuna utengano fulani. Tulipoanza mchakato wa kuanzisha Jumuiya hapa, mchakato huo huo ulianza kwa wanafunzi pia, tuliwapa ofisi hapa ubalozini na kila jumamosi au jumapili walikuwa wakikutana hapa.

Madhumuni makubwa ni kuwataka wajione ni sehemu ya Diaspora wasijitenge nao lakini utakuta wanajifungia wenyewe lakini tunajaribu kuwahamasisha kwamba mkija hapa mjione kuwa ni kitu kimoja tuko pamoja.

Sisi kama ubalozi Mtanzania yeyote tunampa kipaumbele, na wanasema wanachama ni wale wanaolipa ada, lakini sisi tunaamimi yakitokea masuala yoyote tunashirikisha Watanzania wote. Tukiandaa shughuli tunashirikisha Watanzania wote. Sisi tunaamini kuwa kazi ya kujenga Diaspora ni ya muda mrefu.

MTANZANIA: Vipi mnawahamisha Diaspora kuweza kusikika kule nyumbani?

MSEKWA: Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete alipokuja hapa aliwaambia pamoja na jitihada zake na wao wajitahidi na sisi tunawahamisha watafute njia ya kujenga hoja ili wasikike kwa sababu watu wana mambo mengi kule nyumbani na hawaelewi Diaspora.

Kwa hiyo kuwapo makongamano na kuandika makala magazetini ni njia mojawapo ya wao kusikika na watu watawaelewa.

Nakumbuka wakati fulani nilikaa na maofisa fulani hapa tukijadili masuala ya Diaspora, tulijaribu kujenga somo pale na mwisho wa siku wakaniuliza wewe ni Diaspora au, lakini nasema hao ndio watu walio katika ngazi ya uamuzi na hawafahamu umuhimu wa Diaspora lakini hili ni jambo linakwenda hatua kwa hatua hatimaye somo litaeleweka.

Mimi nimewaambia wenzangu nikirudi nyumbani nitakuwa mpiganaji mzuri sana wa masuala ya Diaspora kwa sababu naelewa mchango wao na kwa misingi hiyo taratibu watu wanaelewa.

MTANZANIA: Una wito gani kwa Serikali ya Awamu ya Tano?

MSEKWA: Mimi ni mtumishi wa Serikali siwezi kutoa wito ila nataka kusema mimi ni mtumishi kokote ninakopangiwa kufanya kazi nitakwenda kwa sababu naitumikia nchi yangu. Kazi haina mtu lakini naamimi kwamba shughuli yoyote ni mwendelezo na utekelezaji wa majukumu.

Mimi nafanya kazi hapa ya kumsaidia balozi na muda wangu ukiisha nikihitajika nyumbani nitarudi na atakuja mtu mwingine na ataendeleza kazi niliyoiacha mimi kwa sababu msingi upo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles