27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Mrema ataka Kikwete aongezewe muda

Augustine Mrema
Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema

NA MAREGESI PAUL, DODOMA

MBUNGE wa Vunjo ambaye pia ni Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Augustine Mrema (TLP), amesema kuna haja Rais Jakaya Kikwete aongezewe muda wa kuongoza nchi.

Alisema kama Rais Kikwete ataongezewa muda, atapata muda wa kukamilisha mchakato wa Katiba ambao ndiye aliyeuanzisha.

Mmoja wa wajumbe waliohudhuria kikao kati ya Rais Kikwete na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kilichofanyika mwanzoni mwa wiki Ikulu ndogo ya Kilimani mjini hapa, aliiambia MTANZANIA kwamba Mrema aliyasema hayo alipokuwa akichangia wakati wa kikao hicho.

“Wakati mjadala unaendelea, Mrema alipendekeza Rais Kikwete aongezewe muda wa mwaka mmoja au miwili ili afanikiwe kukamilisha mchakato huu wa Katiba.

“Alipotoa pendekezo hilo, kuna mjumbe mmoja akamuuliza, ‘sasa Mrema unataka muda uongezwe ili na wewe upate muda wa kupambana na Mbatia (James Mbatia, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi) anayekusumbua kule Vunjo au?’

“Huyo mjumbe alipouliza hivyo, Mrema akadakia na kusema, ‘hapo hapo’,” kilisema chanzo chetu kwa sharti la kutotajwa gazetini.

Chanzo hicho kilisema kuwa Mrema aliendelea kumsihi Rais Kikwete amzuie Mbatia asiende Vunjo kwa kuwa anapokuwa huko anatumia jina lake, kwamba amemtuma kugombea ubunge wa jimbo hilo.

Mbatia alipozungumza na MTANZANIA kwa simu jana juu ya malalamiko hayo, alisema hawezi kuendelea kujibizana na Mrema kwa kuwa ni mkubwa wake.

“Mimi sikulelewa katika mazingira ya kujibizana na wakubwa zangu ila ninachosema ni kwamba, wakati wa mkutano wangu wa hadhara niliohutubia Vunjo wiki iliyopita, wenyeviti 11 wa serikali za vijiji walioshinda kupitia TLP, wenyeviti 32 wa vitongoni ambao ni wa TLP, msaidizi wa Mrema pamoja na wanachama wapya 1,564, walihamia NCCR-Mageuzi,” alisema Mbatia.

Naye Mrema alipozungumza na MTANZANIA kwa simu, alikiri kutaka Rais Kikwete aongezewe muda na kumwomba amzuie Mbatia kwenda Vunjo akidai kuwa anatumia jina la rais kumsema vibaya kwa wananchi.

- Advertisement -

Related Articles

1 COMMENT

  1. Kuna watu walitaka MzeeMwinyi aongezewe muda. Mzee Mwinyi akiwa mlezi mkuu wa siasa za vyama vingi hakukubali na hivyo kulinda heshima ya maamuzi ya nchi. Mzee Mkapa naye aliombwa hivyohivyo, naye akaikuza demokrasia zaidi kwa kutokukubali. Rais wetu Kikwete, shujaa wa muungano aliridhia kuweko mchakato wa kuipata katiba iliyoliliwa miaka nenda miaka rudi. Yeye ametimiza hili na anastahili kupongezwa, na zaidi ya hayo, sisi sote ni watanzania, Rais ajaye hatakuwa na ubavu kukataa mjadala wa katiba usiendelee. Baada ya mwaka kesho tumwache Rais wetu apumzike. Hii ya Mbabtia ni vyema Mrema akakumbuka kuwa kwenye siasa hizi za sasa kuongoza jimbo kwa zaidi ya vipindi viwili ni tunu toka kwa Mwenyezi Mungu. Mbatia ni lazma agombee kwa maana keshaingia kwenye siasa, na jinsi sahihi ya kujiwakilisha vyema kisiasa ni kupitia bungeni. Sasa hawezi kuwa na hakika kama mwaka ujao atateuliwa kuwa mbunge naRais ajaye – ni bora “akajaribu” kwa wananchi. Kama tunavyoona haifai kwa Rais kukaa madarakani kwa zaidi ya vipindi viwili iwe hivyo hata kwa wabunge!

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles