27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

MR BLUE SOMA ALAMA ZA NYAKATI, ACHANA NA DIAMOND

Na RAMADHANI MASENGA       

KILA kitu kinawezakana. Amini hivyo kuanzia sasa. Ila usiishie hapo. Amini kila kitu kinawezekana kutegemea na nyakati na mazingira. Usiamini kuwa unaweza kuimba leo na kesho ukawa mwanamuziki mkubwa Afrika na Duniani.

Ila suala hilo linawezekana baadaye kama ukitengeneza mazingira mazuri leo.

  Mr Blue ni kama ana vita baridi na Diamond Plutnumz.  Msikilize katika mahojiano yake, msikilize maoni yake juu ya Diamond. Kuna kitu hakipo sawa kati yao.

     Kuna nyakati aliwahi kusema kila anapopita yeye Diamond naye  hupita. Hapa hakuwa anazungumzia muziki. Alikuwa anazungumzia mapenzi. Alisema alianza kwa Wema Sepetu na Diamond akapita, akaja kwa Naj na hapa Diamond pia akakanyaga. Kwingine sipajui.

    Mr Blue anamuona Diamond katika jicho tofauti na analomuangalia mwanamuziki mwingine. Ni kama hamuamini ama hamuelewi. Ni kama anamchukia ama anachukia mafanikio yake. Msikilize tu Mr Blue dhidi ya Diamond utaelewa nini nina maanisha.

Hisia tofauti za Mr Blue kwa Diamond zinamfanya amsifie sana hasimu wake Ali Kiba kwa kila kitu. Siyo dhambi na wala haikatazwi. Ila ingefaa iishie huko siyo huku anapokuja sasa.

   Diamond anajiita Simba, Mr Blue naye kaibuka na kusema hilo ni jina lake. Siyo mbaya. Huenda ni kweli. Ila ni vema Mr Blue akafahamu sasa kuwa Diamond yuko juu mara nyingi kuliko yeye hivyo kishindo chake ni kikubwa na kinaweza kumpoteza msanii mwingine kama hajajiandaa kupambana naye. Mr Blue ni vema akamuangalia Bob Junior ili apate mfano mzuri.

 Bob Junior alipambana kulitaka jina la Sharobaro ambalo Diamond alisema yeye ndiye mwenye kulistahili. Baada ya mpambano ya maneno kwa muda mrefu, Diamond akaliacha na Bob Junior akaendelea kulitumia.

Ila unaweza kujiuliza kati ya jina la Sharobaro ambalo Bob Junior alikuwa akililia na jina la Wasafi ambalo Diamond aliibuka nalo baada ya kulitema jina la Sharobaro, ni lipi lipo juu zaidi?

Ukipita katika viunga vya wapenda muziki na ukauliza ni msanii gani anajiita Simba, wote watasema Diamond na siyo Mr Blue. Hapa Blue anatakiwa kujifunza kitu. Kama yeye ni wa kwanza kulitumia jina hili, ni kwanini basi lionekane la Diamond na siyo yeye?

Hapa ndipo anatakiwa kujua uzito wa huyu jamaa katika game ya Bongo flavour ni mzito kupita kiasi.

    Mr Blue ni msanii mkali sana. Ana mashabiki wengi na wanamuziki wengi wamekuwa wakiiiga namna yake ya kuimba na hata kuvaa. Ila kwa sasa anatakiwa kujua nyakati hizi siyo salama sana kwake kupambana na Diamond. Diamond ni nyota wa muziki Tanzania na Afrika.

   Mtu anaweza kuwa shabiki wa Mr Blue na akawa shabiki wa Diamond. Ila sio lazima sana shabiki wa Diamond kuwa shabiki wa Blue. Hapa Kabayser anatakiwa kujiuliza na kisha asome alama ukutani kuwa Diamond ni mnyama hatari sana kwa sasa asiyefaa kuchezewa hovyo.

     Mr Blue mbali na kutangulia katika muziki kabla ya Diamond ila kwa sasa ana mengi ya kujifunza kwa huyu Mmanyema wa Madale kuliko kupambana naye. Kupambana na Diamond ni kujiumiza tu na kujinyima fursa ya kuendelea kujifunza mengi.

   Kwa sasa vita ya Diamond na Mr Blue ni sawa na mwalimu na mwanafunzi wake. Mwanafunzi akimnunia mwalimu wake anajikosesha nafasi ya kujifunza mwenyewe bila kuacha athari kwa mwalimu. Ahsante.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles