23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Moyes: Sikuwa natendewa haki Man United

David MoyesLONDON, ENGLAND

KOCHA mpya wa klabu ya Sunderland, David Moyes, amefunguka kwa mara ya kwanza kuelezea maisha aliyokuwa anaishi katika klabu ya Manchester United na kudai kuwa yalikuwa mabaya.

Kocha huyo amesema alikuwa hatendewi haki katika klabu hiyo na ndiyo maana alishindwa kuonesha uwezo wake, lakini kwa sasa yupo sehemu sahihi ambayo ataonesha uwezo wake, tofauti na Old Trafford.

Kocha huyo alisajiliwa na klabu ya Manchester United kwa mkataba wa miaka sita, lakini hakumaliza mkataba huo kwa kuwa alifukuzwa kwa madai kuwa timu ilikuwa inapata matokeo mabaya.

Nafasi ya kocha huyo ikachukuliwa na Louis van Gaal mwanzoni mwa msimu wa 2014-15, lakini na yeye alifukuzwa nafasi hiyo kutokana na mwenendo mbaya wa klabu, ambapo sasa mikoba hiyo ameichukua Jose Mourinho.

“Nilikuwa na lengo la kuipeleka United sehemu sahihi, lakini ilishindikana kutokana na mwenendo wa uongozi wa timu kuwa mbaya, nikashindwa kufanya vile ambavyo nilitarajia kufanya.

“Nilisaini mkataba wa miaka sita, lakini nilitumikia klabu hiyo kwa miezi 10, kutokana na hali hiyo niliamini kuwa kuna jambo ambalo lilikuwa linaendelea.

“Lakini hayo ni maisha ya soka, siku zote ndivyo yalivyo. Kila kocha anakuwa na lengo la kutaka kufanya vizuri akiwa na timu yake, lakini sikuweza kushinda vizuri baadhi ya michezo kutokana na kunyanyaswa.

“Ukweli ni kwamba viongozi wa klabu hiyo walikuwa hawanitendei haki, lakini sehemu niliyopo kwa sasa ninaamini nipo mahali salama na nitafanikiwa kufanya vizuri na kurudisha heshima yangu,” alisema Moyes.

Hata hivyo, kocha huyo amesema kwamba baada ya kuondoka Manchester United alipata ofa mbalimbali katika klabu kubwa, lakini aliamua kujiunga na Real Sociedad kabla ya kujiunga na klabu ya sasa, Sunderland.

Kocha huyo amesema mashabiki wa klabu ya Sunderland watarajie makubwa kwa kipindi cha mkataba wa kocha huyo na anaamini kuwa atafanya ushindani mkubwa dhidi ya makocha ambao wanadhaniwa kuwa watafanya makubwa msimu mpya.

“Ni wazi kwamba ligi itakuwa na ushindani mkubwa msimu mpya, kuna makocha ambao wanazungumziwa kuwa watafanya vizuri, lakini wakumbuke hakuna ambaye alijua kama klabu ya Leicester City itachukua ubingwa msimu uliopita, basi hayo yanaweza kutokea katika msimu mpya wa Ligi.

“Kila kocha ana lengo la kufanya makubwa, hata mimi nina lengo la kushindana na hao ambao wanadhaniwa wanaweza kufanya makubwa,” aliongeza.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles