23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

MKWASA NI ZAIDI YA KATIBU YANGA

Na ADAM MKWEPU- DAR ES SALAAM



KWA ujumla klabu ya soka ya Yanga ipo katika kipindi kigumu na kama si uzoefu wa Katibu Mkuu wa sasa, Boniface Mkwasa, ingeyumba zaidi.


Mkwasa amekuwa Yanga kama mchezaji, baadaye kocha na sasa kiongozi, hivyo anaijua vyema klabu na njia za kupitia kuifanya iende.

Kimsingi kocha huyo amekuja muda mwafaka Yanga, kwani kwa sasa uzoefu wake ndio chachu ya matumaini ndani ya klabu hiyo.

Ndio maana wiki iliyopita Katibu huyo alitamba kuwa klabu hiyo ina utajiri wa kutosha kukabiliana na changamoto zozote bila kutetereka kiushindani katika michezo yao ya Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kwani utajiri huo ndio sababu ya klabu hiyo kutopitisha mchango kwa wanachama wake, wakidai bado wanaweza kulipa mishahara ya wachezaji na viongozi pamoja na gharama za michezo ya nyumbani na ugenini ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Wanatarajia kulipa madeni ya mishahara ya Januari, mwaka huu kwa wachezaji na wafanyakazi wote wa klabu hiyo.

Siku zinaenda na Yanga haijakwama. 
Pamoja na hayo, kwa hali ambayo inaikabili klabu hii leo wa kulaumiwa ni wana Yanga wenyewe kuruhusu klabu imtegemee mtu mmoja (mwenyekiti).


Lakini kama klabu ingekuwa na vyanzo vingine vya mapato kama wadhamini na vitega uchumi isingeyumba kiasi kinachozungumzwa leo.

Mkwasa amejitahidi kuweka Yanga kwenye ramani, vinginevyo tungeviona vioja tulivyovisahau vya wanachama na mashabiki wa klabu hiyo kutofautiana na kulumbana.

Katibu huyo anafahamu kabisa kwamba viongozi wakijaribu kutofautiana wanawapa nafasi wapinzani wao Simba kujitangaza kuwa mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara mapema.

Kwa kulitambua hilo, hakuona ugumu wa kuthubutu kuwaaminisha mashabiki wa timu hiyo kwamba fedha zipo na kila kitu ndani ya klabu kipo sawa.

Kila mtu anafahamu ukweli halisi ndani ya klabu hiyo baada ya Mwenyekiti wake kupata matatizo ya kiuchumi.

Kitendo hicho ndio sababu ya baadhi ya wachezaji wa kigeni kuwa mbioni kuondoka kutokana na sababu za masilahi, miongoni mwao ni beki Mtogo, Vicent Bossou na mshambuliaji Mzimbabwe, Donald Ngoma.

Mbali na Mwenyekiti wa klabu hiyo kuwa mfadhili mkubwa, wsakati fulani Yanga ilipata udhamini wa Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) uliodumu kwa takribani miaka 10 ambao ulisaidia sana klabu hiyo kifedha.

Pamoja na mgogoro uliojitokeza mwaka jana hadi Yanga kuachana na TBL, lakini tayari kampuni hiyo ya bia ilikwishapanga kuacha kuidhamini klabu hiyo na mahasimu wao, Simba na ndiyo maana hata zile mechi za Nani Mtani Jembe zilikufa.


Ni jambo la muda tu kuona mabadiliko makubwa yatakayotokana na Mkwasa ikiwamo kurejesha umoja wa wanachama na kuongeza hamasa kwa wachezaji na mashabiki.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles