24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

MKOSOAJI WA SERIKALI YA URUSI AUAWA UKRAINE

KIEV, UKRAINE


POLISI nchini Ukraine imesema mwandishi habari wa Urusi aliyekuwa akifanya kazi katika chombo cha habari cha upinzani, Arkadi Babchenko, ameuawa kwa kupigwa risasi mjini hapa jana.

Akizungumza na Shirika la Habari la Ufaransa (AFP), msemaji wa polisi, Yaroslav Trakalo, alisema Babchenko alikutwa chumbani na mke wake akivuja damu baada ya kusikia milio ya risasi.

Hata hivyo, mwandishi huyo alifariki dunia wakati akiwa kwenye gari la kubebea wagonjwa akikimbizwa hospitalini.

“Arkadi Babchenko aliuawa kwa kupigwa risasi tatu mgongoni mwake alipokuwa anapanda ngazi nyumbani kwake baada ya kutoka dukani,” alisema mwanahabari mwenzake Osman Pashayev, kupitia ukurasa wake wa Facebook.

Mkosoaji huyo mkubwa wa Rais Vladimir Putin, amekuwa akiendesha kipindi katika televisheni binafsi ya Ukraine ya ATR kwa mwaka mmoja sasa baada ya kuondoka Urusi Februari mwaka jana.

Babchenko (41) aliondoka Urusi baada ya kupokea vitisho kufuatia hatua yake ya kuikosoa nchi hiyo juu ya jukumu lake katika mgogoro wa mashariki mwa Ukraine, akiishutumu kutoa msaada wa kijeshi kwa waasi.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Polisi mjini Kiev, Andriy Kryshchenko, mwandishi huyo ni mkosoaji wa pili wa Urusi aliyekimbilia hapa kuuawa kipindi cha chini ya miaka miwili huku akisema wanashuku kuuawa kwake kunatokana na kazi yake.

Aidha msaidizi katika Wizara ya Ndani ya Ukraine, Anton Guerachchenko, moja kwa moja ameinyooshea kidole Urusi kuhusika na mauaji hayo.

Guarachchenko aliandika kwenye ukurasa wake wa Facebook, akisema Serikali ya Rais Putin inawalenga wale isioweza kuwavunja au kuwatisha.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi, Sergei Lavrov, amekanusha madai hayo huku akitaka uchunguzi wa kina kufanyika juu ya mauaji ya Babchenko.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles