30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MKAPA: VIONGOZI KUWENI WASIKIVU

* Warioba asema kiongozi bora anapaswa kuheshimu kila mtu


Na ASHA BANI

RAIS mstaafu Benjamin Mkapa, amesema mambo matatu ya kuzingatia katika uongozi bora ni kuwa msikilizaji wa watu, mvumilivu na kupenda kusoma mambo ya ndani na nje ya nchi.

Mkapa aliyasema hayo jana, wakati wa kongamano maalumu la maadhimisho ya kumbukizi ya Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere yaliyofanyika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kigamboni, Dar es Salaam.

Katika kongamano hilo, Mkapa alimwakilisha Rais Dk. John Magufuli.

Alisema katika mambo matatu ya kuyakumbuka na kuyaenzi katika uongozi wa Mwalimu Nyerere, huku akiwataka viongozi wengine kuiga mfano huo, ni usikivu na kushirikisha watu wengine kupata maoni mbalimbali ya kujenga nchi.

Mkapa alisema Mwalimu Nyerere alikuwa anawasikiliza watu, hata wale ambao walikuwa wanampinga na  wanaomuunga mkono.

Alisema alikuwa kiongozi anayependa kujifunza na kusoma mambo ya ndani ya nchi na nje kwa lengo la kufahamu historia mbalimbali.

Kutokana na hilo, aliiomba Serikali kuanzisha mitaala itakayokuwa inatoa elimu ya historia ya nchi kuanzia elimu ya chini hadi ya vyuo vikuu.

“Utashangaa mtu wa chuo kikuu hajui historia ya mtu, wala hajui kiongozi kama Mfaume Rashid Kawawa alikuwa ni nani katika taifa hili… hii ni aibu,” alisema.

Mkapa alisema tangu Mwalimu Nyerere alipofariki dunia, nchi imekuwa na changamoto nyingi ambazo zinahitajika kujipanga ili kukabiliana nazo.

Alisema kunatakiwa kuwa na mpango wa kutoa elimu ya maadili kwa viongozi wa umma.

 

JAJI WARIOBA

Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba, akichangia mada ya siasa safi na uongozi bora, alisema kiongozi bora ni mzalendo, mchapakazi, mcha Mungu na anayemheshimu kila mtu kwa kuwa kila binadamu ana haki ya kuheshimiwa.

Alisema katika vitu hivyo vyote, Mwalimu Nyerere alikuwa navyo na ndiyo maana viongozi waliopitia kwenye mikono yake wengi wao wamekuwa waadilifu.

Jaji Warioba alisema kiongozi anatakiwa kufahamu maisha ya watu anaowaongoza, kwa sababu Nyerere alikuwa akifanya hivyo.

“Nyerere alikuwa akizunguka huko na huko kuangalia wananchi wake wanaishije, maisha ya Watanzania yanaonekana pale ambapo utawangalia, utakuta wamevaa nguo zimepasuka, wanatembea wakiwa wamevaa kandambili.

“Mwalimu Nyerere, nyakati za jioni alikuwa anatoka kucheza bao na wananchi wake na wazee, huku akibadilishana nao mawazo ya hapa na pale, kitendo hiki kilikuwa kikimsaidia kupata mawazo kutoka kwa wananchi,” alisema.

Jaji Warioba alisema kiongozi bora ni yule ambaye anaweza kusikiliza nyimbo, ngonjera zikiwa na ujumbe mbalimbali ambazo zinawakilisha matatizo ya wananchi.

Alisema siku zote kiongozi bora anaomba ushauri kwa watu.

“Hata wakati wa utawala wake, Mwalimu Nyerere aliweza kupokea ushauri wakati akiongoza Baraza la Mawaziri.

 

JOSEPH BUTIKU

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku, alisema nchi inavunja Katiba kutokana na mambo mbalimbali yanayoendelea, ikiwa ni pamoja na vitendo vya rushwa katika siasa.

Alisema Zanzibar, Tanzania Bara wanavunja Katiba kutokana na kushindwa kuheshimu sheria na vifungu walivyojiwekea.

 

PHILIP MANGULA

Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara),Philip Mangula, akichangia mada inayohusu maadili ya viongozi, alisema wakati wa utawala wa Mwalimu Nyerere walikuwa wazalendo kutokana na kufanya kazi kwa kujishusha kwa wananchi na kuwasikiliza matatizo yao.

Alisema hata viongozi waliokuwa wakipewa nyadhifa mbalimbali, walikuwa wakifuatiliwa nyendo zao, ikiwa ni pamoja na kufanya kazi kwa kupinga udini, ukabila na rushwa.

 

MJENGI GWAO

Aliyewahi kuwa kiongozi ndani ya CCM katika nafasi mbalimbali, Mjengi Gwao, alisema chama hicho kimeporomoka katika maadili ya viongozi.

Alisema chama kimekuwa na viongozi wa ajabu ajabu walioingia katika uongozi huo kiujanja ujanja kwa utaratibu usiofaa.

Gwao alisema kutokana na kugundua hali hiyo, aliwahi kumwandikia maelezo Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana na Mangula ili wafanye marekebisho ya haraka.

 

JOHN CHEO

Mwenyekiti wa Chama cha UDP, John Cheo, aliomba Serikali kukifanya chuo hicho kuwa cha kitaifa na si cha kisiasa.

Alisema ni vyema vyama vya siasa kupanga jinsi ya kuendesha nchi, ikiwa na mfumo wa vyama vingi bila kupigana wala kuvuruga amani.

 

EDA SANGA

Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), Eda Sanga, alisema jamii imeingia katika kufanya vitendo vya ukatili ikiwa ni pamoja na ubakaji, ulawiti hivyo katika kumuenzi Mwalimu Nyerere ni vyema kuhakikisha maadili ya jamii yanarudi katika hali yake ya kawaida.

 

JAJI RAMADHANI

Jaji Mkuu mstaafu, Augustino Ramadhani, alisema haki za binadamu zinatakiwa kujulikana na kila mtu.

Alisema kila mtu anatakiwa kufahamu haki zake na viongozi wanatakiwa kuheshimu na kutekeleza kwa vitendo.

 

JOSEPH MWANGOSI

Kiongozi kutoka chama cha Sauti ya Umma, Joseph Mwangosi, alisema nchi imeporomoka maadili na utu kutokana na vitendo vya utekaji vinavyoendelea bila kuwa na majibu sahihi kutoka serikalini.

 

RENATUS MUHABI

Kiongozi wa Chama cha Kijamii (CCK), Renatus Muhabi, alisema ili mambo katika nchi yaende sawa, ni lazima kurudishwa kwa mchakato wa katiba mpya.

 

SAMWELI KASORI

Akiwakilisha mada ya uzalendo na uadilifu katika taifa, Samuel Kasori ambaye aliwahi kuwa msaidizi wa Mwalimu Nyerere, alisema uadilifu wa viongozi unajengwa na uwajibikaji na utendaji, ikiwa ni pamoja na viongozi kuwatumikia wananchi.

 

POLEPOLE

Katibu wa NEC, itikadi na Uenezi (CCM), Humphrey Polepole, alisema viongozi ndani ya CCM watahakikisha wanarudisha chama katika nidhamu na kwamba wanatakiwa kuwa na maadili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles