33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Mitambo ya kupima tetemeko yaibwa

Darasa la Shule ya Sekondari ya Ihungo iliyopo Bukoba likiwa limebomoka kutokana na tetemeko lililotokea mwishoni mwa wiki.
Darasa la Shule ya Sekondari ya Ihungo iliyopo Bukoba likiwa limebomoka kutokana na tetemeko
lililotokea mwishoni mwa wiki.

* Vituo 38 vyafungwa baada ya wafadhili kuondoka 

* Wananchi Bukoba walilia misaada, tetemeko laendelea  kutikisa

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

WAKATI taifa likiwa katika majonzi kutokana na vifo 16 vilivyotokana na tetemeko la ardhi na kuacha majeruhi zaidi ya 253 mkoani Kagera wiki iliyopita, siri ya kushindwa kupimwa matetemeko nchini imebainika.

Imeelezwa kuwa vituo vitatu vikubwa vya kupima matetemeko   vimefungwa baada ya kuhujumiwa na vingine vidogo 38 navyo vimefungwa baada ya wafadhili kujitoa.

Hayo yalielezwa  jana na Jiolojia Mwandamizi wa Wakala wa Jiolojia Tanzania, Gabriel Mbogoni alipozungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu.

“Kwa kweli wanajiolojia tunapata changamoto kubwa katika kupima na  kujua iwapo tetemeko litatokea katika eneo fulani na hiyo inatokana na kuhujumiwa  baadhi ya mashine katika vituo vyetu.

“Tulikuwa na vituo zaidi ya 10 vya kupima matetemeko, hivi sasa  vimebaki tisa pekee  na ili kupata uhakika kama kuna tetemeko kwenye eneo fulani lazima uwe na vituo zaidi ya vitatu,” alisema.

Alisema vituo vilivyofungwa baada ya   kuibwa  vilikuwa katika mikoa ya Morogoro, Dodoma (Ntuka) na Arusha  eneo la Longido.

“Ili tuweze kusimika mashine za kupima tetemeko tunahitaji kupata eneo ambalo lina mwamba mgumu.

“Zamani tulikuwa tukitafuta maeneo yenye miamba migumu huko vijijini, tukipata tunawasiliana na viongozi wa kijiji na tunaweka walinzi wa kulinda mashine hizo.

“Lakini zimeibwa hali iliyosababisha kufungwa   vituo hivyo…tulipeleka kesi mahakamani mwisho tukaona ni vema sasa tuanze kuzifunga mashine hizo katika maeneo ya magereza kwa usalama wake isipokuwa kile cha Mtwara na Dodoma,” alisema.

Alisema wezi hao, wamekuwa wakiiba mashine hizo wakidhani  wanaweza kunufaika, wakizifananisha na madini.

“Wengi wanadhani zinamilikiwa na Wizara ya Nishati na Madini kwamba wakiziiba watauza wapate faida.  Unajua mashine hizi zipo kama sanduku, wanapoziiba huwa hawawezi kuziuza popote kwa sababu zinatambulika,” alisema.

Mbogoni alisema vituo vikubwa vilivyobakia vipo katika mikoa ya  Mtwara, Dodoma, Geita, Arusha, Babati, Singida, Mbeya na Manyara.

Akizungumzia  vituo vidogo 38 vilivyofungwa, alisema hiyo ilitokana na kumalizika  mradi wa kupima matetemeko uliokuwa ukifanywa na wakala huo kwa kushirikiana na Chuo cha Pennyslvania State cha Marekani.

“Siwezi kutaja tumepata hasara kiasi gani kwa sababu sijui mashine hizo zilinunuliwa kiasi gani na sasa zinauzwa kiasi gani. Huwa tunazipata kutoka  kwa ufadhili wakati wa utekelezaji wa miradi mbalimbali.

“Awamu ya kwanza wa mradi ulianza 2007 hadi 2008 halafu ukaanza tena 2013 hadi April 2015 ambako uliisha,” alisema.

Mbogoni alisema matetemeko mengine madogo yataendelea kutokea kwa muda.

“Ni hali ya kawaida linapotokea tetemeko kubwa huwa baadaye yanatokea mengine madogo madogo, yanaweza yakadumu hata kwa wiki au hadi miezi minne.

“Hii ni kwa sababu ile nguvu ya mgandamizo inayotokea ambayo husababisha miamba kumeguka huwa bado haijaisha na ndiyo maana tetemeko huendelea kutokea,” alisema.

Juzi, tetemeko kubwa lilitokea katika maeneo ya Kanda ya Ziwa hususan mkoani  Kagera lilisababisha zaidi ya vifo 15 huku likiacha majeruhi zaidi ya 253.

Tetemeko hilo limesababisha maelfu ya wananchi kukosa makazi baada ya nyumba 840 kuanguka na nyingine 1,264 kupata nyufa, yakiwamo majengo 44 ya taasisi mbalimbali za umma.

WANANCHI

Wakati huohuo, baadhi ya wananchi walioathirika na tetemeko la ardhi  mkoani Kagera wiki iliyopita  wameiomba Serikali kuwasaidia kujenga mahema haraka  weweza kujihifadhi kutokana na nyumba zao kuanguka

Wakizungumza na MTANZANIA kwa nyakati tofauti mjini Bukoba jana, wananchi hao walisema hivi sasa wanalazimika kulala nje bila kuwa na kitu chochote cha kuwahifadhi.

Mmoja wa wananchi hao, Evodius Gozbert mkazi wa Bukoba mjini, alisema anakabiliwa na hali ngumu kutokana na nyumba yake yote kubomoka.

“Nimepoteza nyumba zangu, tunahitaji msaada wa haraka kutoka serikalini, wasiwasi wetu hapa mvua ikianza kunyesha tutakimbilia wapi.

“Kama ulivyosikia juzi saa 4.00 usiku na jana asubuhi tetemeko lilijirudia, hii inaonyesha wazi bado lipo, lazima tuwe na sehemu za kijikinga ndugu yangu,”alisema

Naye Joyce Ndukeke alisema tangu kutokea tetemeko   hadi jana jioni alikuwa hajapata msaada kutoka serikalini.

“Mimi ni mzazi wa watoto wanne, nyumba zote zimeanguka, nasikitika mume wangu yuko safarini, hatuna pa kulala hapa si umeona limejirudia tena, hapa tumetawaliwa na hofu,”alisema.

Mutalemwa Emmanuel  alisema wamekumbwa na hofu kubwa kwa sababu  hata wanashindwa kutafuta vyumba vya kupanga katika nyumba nyingine, kwa sababu nazo zinaweza kuanguka.

Naye Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Rwome, Ashiraph Alphonce alisema wameanza kuzungukia maeneo yote kuorodhesha nyumba zoye zilizobomoka na zile zenye nyufa.

“Tunapita  kwenye mtaa wangu kuona nyumba zilizoanguka, mpaka leo (jana) nimehakiki kaya 58.

“Naiomba Serikali ilete msaada wa haraka kwa wananchi kwa sababu hadi sasa hakuna msaada wowote, wananchi wanaangaika wenyewe, tunaomba angalau wapatiwe mahema wapate pa kuishi,” alisema Alphonce.

DC

Akijibu malalamiko ya wananchi hao, Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Deodatus Kinawiro, amewataka wawe watulivu wakati huu ambao Serikali inaendelea na kazi ya kuhakiki ili wapate msaada haraka iwezekanavyo.

“Nimeunda kamati ya kufuatilia wananchi walioathirika wale walengwa kabisa, mpaka sasa kwenye wilaya yangu kuna watu kama 3,000 hawana makazi,” alisema.

RC KIJIU

Mkuu wa Mkoa wa Kagera,Meja Jenerali Salum Kijuu alisema  mpaka jana mchana hakuna vifo vilivyoongezeka ingawa majeruhi waliokuwa wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wamepungua kutoka 253 hadi 61.

Alisema hakuna upungufu wa dawa na vifaa tiba vingine vinavyohitajika na   huduma inaendelea kutolewa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles