24.4 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

MISS TANZANIA ACHOKA KUKAA GEREZANI

 

PATRICIA KIMELEMETA NA MANENO SELANYIKA

ALIYEKUWA mrembo wa Tanzania mwaka 1996, Shose Sinare, ameuomba upande wa mashtaka kuwasilisha mawasiliano yanayofanyika kutoka Tanzania na Uingereza katika kesi ya utakatishaji wa fedha inayomkabili yeye na wenzake wawili.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni pamoja na aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya na aliyekuwa Mwanasheria wa Benki ya Stanbic, Sioi Solomon.

Sinare alidai hayo jana, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mbele ya Hakimu Mfawidhi, Cyprian Mkeha na kuuomba upande wa Jamhuri kuleta mawasiliano hayo, kwa kuwa tayari wamekaa gerezani mwaka mmoja na nusu, hivyo upande wa mashtaka uwasilishe mawasiliano hayo.

Awali, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mutalemwa Kishenyi, alidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kwamba wanasubiri awamu ya pili ya upelelezi huo.

Hata hivyo, Hakimu Mkeha aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 25, mwaka huu, ili upande wa mashtaka ueleze mwendelezo wa kile kilichowasilishwa mahakamani hapo jana.

Awali, washtakiwa hao walipandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka, likiwamo la kula njama, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kutakatisha fedha.

Wanadaiwa kuwa, makosa hayo waliyatenda kati ya Machi 2013 na Septemba 2015, wakati wa mchakato wa mkopo wa dola za Marekani milioni 550 kwa Serikali ya Tanzania kutoka Benki ya Standard Chartered ya Uingereza.

Wanadaiwa kuwa Agosti 2, 2012, Sinare kwenye Makao Makuu ya benki ya Stanbic iliyopo Kinondoni, kwa nia ya kudanganya aliandaa nyaraka ya mapendekezo akijaribu kuonyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingereza ikishirikiana na benki ya Stanbic ya Tanzania watatoa mkopo wa dola za Kimarekani milioni 550 kwa Serikali ya Tanzania kwa ada ya uwezeshaji ya asilimia 2.4 ya kiasi cha mkopo huo, wakati akijua kuwa si kweli.

Inadaiwa kuwa Agosti 2, 2012, Sinare alitoa nyaraka za uongo za mapendekezo ya kuonyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingireza ikishirikiana na Benki ya Stabic ya Tanzania, watatoa mkopo wa dola za Kimarekani milioni 550 na kuziwasilisha katika ofisi za Wizara ya Fedha, wakati akijua kuwa si kweli.

Anadaiwa kuwa, Septemba 20, 2012, katika Makao Makuu ya Benki ya Stanbic nchini yaliyopo Kinondoni, alitenda kosa la kughushi barua.

Sinare anadaiwa kughushi barua ya mapendekezo ikionyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingireza, ikishirikiana na Benki ya Stanbic  ya Tanzania  watatoa mkopo wa dola za Kimarekani milioni 550 kwa Serikali  ya Tanzania kama ada ya uwezeshaji wa asilimia 2.4 ya kiasi cha mkopo huo wakati akijua kuwa si kweli.

Agosti 21, 2012, Sinare anadaiwa kuwa kwa lengo la kulaghai aliwasilisha nyaraka hizo za uongo kuiwezesha Serikali ya Tanzania kupata mkopo huo wa kiasi hicho cha ada ya uwezeshaji, katika ofisi za Wizara ya Fedha.

Washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kughushi nyaraka za makubaliano kwamba  Novemba 5, 2012 katika Benki ya Stanbic, makao makuu Kinondoni, Dar es Salaam, kwa nia ya kudanganya walighushi waraka wa makubaliano wa Novemba 5, 2012.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles