24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mgombea mwenza CUF ataka rasilimali za nchi zitumike kikamilifu

Na MOHAMED HAMAD -KITETO

MGOMBEA mwenza wa urais wa Chama cha Wananchi (CUF), Hamida Abdallah amesema kutotumika kikamilifu rasilimali za Tanzania, kumefanya nchi kuwa na madeni sambamba na kukithiri kwa umaskini wa kipato kwa wananchi wake kila kukicha.

Akizungumza katika kampeni zake mjini Kibaya wilayani Kiteto mkoani Manyara, Hamida alisema rasilimali za Tanzania zinanufaisha baadhi ya watu ambao wanajiita watu maalumu na kuwafanya wananchi kuwa na maisha duni ya kurithishana.

“Miaka mitano chini ya Serikali ya CCM, kipigo chake kila mmoja yuko hoi, nyang’anyang’a, ndembendembe, kifo cha mende mlalo wa chale. Niambieni sasa mnaonaje,” alisema Hamida.

Alisema Watanzania wafikirie kwa nini wao ni maskini wa kipato wakati kuna rasilimali nyingi na za kutosha.

“Why not, kwa nini vijana wetu wakose ajira wakati rasilimali zipo?” alihoji.

Aliwataka wananchi waendelee kujiuliza kwanini wanaishi nyumba hazina umeme, wanaishi nyumba za kipanga hadi leo, kwanini watoto wao wanasoma shule wakiwa wamekaa chini bila viti wala meza darasani.

Alisema Ilani ya CUF imesheheni mambo mengi ambayo ni ufumbuzi wa matatizo ya wananchi kama vile utatuzi wa migogoro ya ardhi, upatikanaji wa huduma za afya, maji na elimu bure.

Aliwaomba wananchi kumchagua Profesa Ibrahim Lipumba ambaye ni mbobevu wa masuala ya uchumi na ambaye bado anatumika Uganda kama mshauri mkuu katika sekta hiyo awe Rais wa Tanzania.

Kwa upande wake, Ibrahimu Msindo, mgombea Ubunge Jimbo la Kiteto, alisema anataka kuongoza wananchi wa Kiteto na sio makundi ya watu, anataka kuongoza wananchi wenye uchumi mzuri kwa sababu inawezekana kwa rasilimali zilizopo humo.

“Nafahamu Kiteto ni eneo ambalo lina rasilimali nyingi ardhi, madini yanatosha kuwaondolea hali ngumu mliyonayo, chagueni CUF mpate utawala wenye tija, tukatae umaskini kwa kusema hapana,” alisisitiza Hamida.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles