27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Mfumuko wa bei wapaa

NA EVANS MAGEGE
WAKATI thamani ya shilingi ikiendelea kuporomoka katika soko la fedha za kimataifa, mfumuko wa bei za bidhaa nao umepaa kutoka asilimia 4.3 hadi 4.5.
Taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa waandishi wa habari ilieleza kuwa mfumuko wa bei kwa mwezi Aprili mwaka huu umepaa kwa sababu ya ongezeko la bei za bidhaa za vyakula na vinywaji baridi.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii, Ephraim Kwesigabo, alisema ungezeko hilo limefikia asilimia 7.1 kutoka asilimia 5.9 ya mwezi Machi mwaka huu.
Kwesigabo alisema kuwa fasihi za bei zimeongezeka na kufikia 157.31 kwa mwezi Aprili mwaka huu, ambapo Aprili mwaka jana kiwango kilifika 150.50.
“Kuongezeka kwa mfumuko wa bei wa mwezi Aprili mwaka huu kumechangiwa hasa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula kwa kipindi kilichoishia mwezi Aprili, zikilinganishwa na bei za mwezi Aprili mwaka 2014,” alisema.
Mkurugenzi huyo alitoa mfano wa mwenendo wa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula zilizoonyesha kuongezeka mwezi Aprili mwaka huu kwa kulinganisha na bei za Aprili mwaka jana, ambapo bei ya mchele imeongezeka hadi asilimia 23.3, unga wa muhogo asilimia 8.4, nyama asilimia 4.9, samaki asilimia 5.8, maharage asilimia 6.8, choroko asilimia 13.3 na sukari asilimia 5.6.
Aidha, alizungumzia mfumuko wa bei kwa kipimo cha mwezi, alisema mwezi Aprili mwaka huu umepimwa kwa kipimo hicho na kuonyesha ongezeko la asilimia 0.8, ikilinganishwa na asilimia 0.7 ya mwezi Machi mwaka huu.
Alisema kuwa fahirisi za bei zimeongezeka hadi kufikia kiwango cha 157.21 kwa mwezi Aprili mwaka huu kutoka katika kiwango cha 155.88 cha mwezi Machi.
Alitaja sababu ya kuongezeka kwa fahirisi hizo kuwa kumechangiwa na ongezeko la bei za bidhaa za vyakula.
“Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa fahirisi ni pamoja na mchele kwa asilimia 5.8, mahindi kwa asilimia 6.3, unga wa mahindi kwa asilimia 5.0, samaki waliokaushwa asilimia 3.1, maharage asilimia 2.9, viazi mviringo asilimia 7.0, mihogo asilimia 6.4 na viazi vitamu asilimia 4.0.
Akizungumzia thamani ya shilingi kwa mwezi Aprili mwaka huu kwa kulinganisha na Septemba 2010, alisema kuwa uwezo wa shilingi 100 kununua bidhaa na huduma umefikia shilingi 63.61 kutoka Septemba 2010, ikilinganishwa na shilingi 64.15 ya Machi, mwaka huu.
Awali akizungumzia hali ya mfumuko wa bei kwa baadhi ya nchi za Afrika Mashariki, alisema umeongezeka kwa nchi tatu za jumuiya hiyo alizozitaja kuwa ni Kenya na Uganda pamoja na Tanzania.
“Mfumuko wa bei kwa mwezi Aprili mwaka huu kwa upande wa Uganda umeongezeka hadi asilimia 3.68 kutoka asilimia 1.90 mwezi Machi, Kenya umefikia asilimia 7.08 kutoka kiwango cha asilimia 6.31 Machi mwaka huu,” alisema Kwesigabo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles