Na Magreth Kinabo – Mahakama ya Tanzania
WIKI iliyopita katika mfululizo wa makala hii ya Siku ya Sheria, tuliishia pale ambapo Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, Mama Bella Bird akisema kuwa ni jambo lisilokubalika kuona Watanzania wengi kwao kupata huduma za mahakama ni kama jambo la anasa.
Alisema; “hii lazima ibadilike kwa sababu Mahakama ni sehemu muhimu katika maisha yao na ustawi wao” anasema Mama Bird.
Anaongeza kuwa, wakati uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi, ni mfumo bora wa utoaji haki ndio utakaotoa mazingira ya uchumi huo kuendelea kukua kwa haraka.
Akizungumzia kuhusu kusogeza huduma za mahakama kwa jamii, Kaimu Jaji Mkuu huyo anasema Mahakama Kuu zinatakiwa kuwa 26, hivyo kwenye kila ngazi ya mkoa, kwa sasa zipo mahakama kuu kwenye kanda 14 tu.
Aidha, Profesa Juma aliitaja mikoa 12 isiyokuwa na mahakama kuu ambayo ni Songwe, Katavi, Njombe, Lindi, Kigoma, Mara, Singida, Morogoro, Pwani, Simiyu, Geita na Manyara.
Hivyo, kutokana na hali hiyo wananchi wa mikoa ya Geita na Mara wanaotafuta haki mahakama kuu, wanatakiwa wasafiri hadi Mwanza. Pia wa upande wa Morogoro na Pwani wanaotaka huduma ya Mahakama Kuu, itabidi wafike Dar es Salaam.
Yule wa Singida ataifuata mahakama kuu Dodoma. Mwananchi wa Katavi hana budi kwenda Sumbawanga kufungua shauri mahakama kuu. Na wa Lindi hufuata huduma ya mahakama kuu Mtwara.
Kwa upande wa mahakama za wilaya, kati ya wilaya 139 zilizopo, ni wilaya 113 tu ndizo zenye mahakama za wilaya na 84 kati ya hizo mahakama hazina majengo yake.
Anasema kuna upungufu mkubwa wa majengo ya mahakama za mwanzo kwenye zaidi ya 3,003 pamoja na nyumba za majaji, nyumba za mahakimu na nyumba za kufikia majaji (Judges Lodge), angalau kila mkoa.
Mpango wa maendeleo ya miaka mitano umedhamiria kukubaliana na changamoto zote tajwa hapo juu.
Hivi sasa katika kukabaliana na tatizo hilo, mahakama kwa kushirikiana na usimamizi wa Wakala wa Majengo (TBA), Chuo Kikuu cha Ardhi, Baraza la Ujenzi la Taifa (NCC) na Benki ya Dunia na Wadau wengine wanaendeleza kukamilisha miradi ya ukarabati na ujenzi wa mahakama kuu Mbeya na mahakama kuu za mikoa ya Kigoma, Mara, Tanga, Dar es Salaam, Arusha, Morogoro, Mwanza na Jengo la Dodoma zitakamilika ndani ya miezi 24.
Ndani ya miezi 6-12 ijayo tutakamilisha ujenzi wa mahakama za hakimu mkazi sita ambazo ni za Manyara, Geita, Simiyu, Njombe, Katavi na Lindi.
Aidha, mahakama za wilaya 19 za mahakama za mwanzo 36 zitajengwa na kukamilishwa katika kipindi cha kufikia Desemba, mwaka huu. Hii ni pamoja na ujenzi wa nyumba za kuishi majaji unaofanywa na Wakala wa Majengo (TBA) kwenye mikoa mbalimbali nchini.
Hatua hii italeta mabadiliko makubwa ya miundombinu ya mahakama na kuweka historia ya upatikanaji wa miundombinu kwa wingi na kwa kipindi kifupi.
Profesa Juma anafafanua kwamba ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi, mahakama itatumia mabasi na boti katika kipindi cha mwaka ujao kama ilivyo katika nchi za Kenya na Uganda.
“Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka mitano (2016/17 – 2020/21) na Mpango Mkakati wa Mahakama 2015/16 – 2019/20.