27.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Meneja kampuni inayojenga SGR apigwa faini Sh milioni 100

Kulwa Mzee – Dar es Salaam

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, imemtia hatiani  Meneja Uwezeshajii wa Kampuni ya Yapi Markezi inayojenga reli ya Standard Gauge, Yetkin Mehmet kwa kosa la kushindwa kutoa maelezo ya Dola za Marekani 84,850 (Sh milioni 195.48) alizokutwa nazo uwanja ndege.

Mshtakiwa huyo ambaye ni raia wa Uturuki, ameamriwa kulipa faini ya Sh milioni 100 na fedha alizokutwa nazo zimetaifishwa na kuwa mali ya Serikali.

Mshtakiwa huyo alifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jana na kusomewa mashtaka yanayomkabili mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba.

Akisoma mashtaka, Wakili wa Serikali Mkuu, Shadrack Kimaro alidai Februari 13 mwaka huu katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, mshtakiwa alikutwa na dola za Marekani 84,850 ambazo alishindwa kuzitolea maelezo kinyume na sheria.

Mshtakiwa anadaiwa alikuwa akisafiri kuelekea Uturuki kwa ndege ya Shirika la Ndege la Turkish.

Mshtakiwa alikiri kutenda kosa hilo na Mahakama ikamtia hatiani kwa kosa moja.

Akiwasilisha hoja ili mshtakiwa apewe adhabu, Kimaro alidai ni mkosaji wa mara ya kwanza hivyo aliomba apewe adhabu kwa mujibu wa sheria.

Wakili wa utetezi, Augustine Shio aliiomba mahakama impe adhabu ndogo mshtakiwa sababu ni mkosaji wa mara ya kwanza na anategemewa katika ujenzi wa reli ya Standard Gauge akiwa Meneja Uwezeshaji.

Hakimu Simba alisema kazingatia hoja za pande zote mbili, hivyo mahakama  inampa adhabu mshtakiwa ya kulipa faini Sh milioni 100 na akishindwa ataenda jela miaka mitatu.

Mahakama pia imeamuru Dola za Marekani 84,850 alizokutwa nazo zitaifishwe na kuwa mali ya Serikali. Mshtakiwa anahangaika kulipa faini ili kunusurika na kifungo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles