Mwandishi Wetu, Dar es Salaam    Â
Mbunge wa Monduli, Julius Kalanga (Chadema) amekanusha taarifa za kuhama chama hicho na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Taarifa za kuhama Chadema zilianza kusambaa leo katika baadhi ya mitandao ya kijamii huku Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema), akiandika katika ukurasa wake wa Twitter kumtakia safari njema huko aendako akimaanisha CCM.
Kalanga anadaiwa kuwaaga baadhi ya viongozi wa Chadema ambapo pia alitarajiwa kutangaza uamuzi huo wa kujiunga na CCM kesho Jumanne Julai 31, jijini Arusha.
Hata hivyo, akizungumza na Mtanzania Digital kwa njia ya simu, Kalanga amesema hana mpango huo na kuongeza kuwa bado yupo sana Chadema.
“Huo ni uzushi tu, hata jana walisema Sumaye (Waziri Mkuu mstaafu na Mjumbe wa Kamati ya Chadema, Fredrick Sumaye) anaondoka leo, mbona bado yupo? ni uzushi tu, sina mpango huo,” amesema Kalanga.