24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Mbunge wa Afrika Mashariki auawa Burundi

Hafsa Mossi
Marehemu Hafsa Mossi

BUJUMBURA, BURUNDI

MBUNGE wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) wa Burundi, Hafsa Mossi, amepigwa risasi na kuuawa na watu wasiojulikana mjini Bujumbura jana.

Mossi, ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Masuala ya Afrika Mashariki katika Serikali ya nchi hiyo, aliuawa nje ya nyumba yake katika barabara ya Gihosha, eneo la Nyankoni.

“Alikuwa garini karibu na nyumbani kwake wakati gari lenye vioo vya giza lilipomgonga kwa nyuma, alishuka kwenda kuangalia kilichotokea na kuishia kupigwa risasi mara mbili,” alisema ndugu mmoja wa karibu.

Msemaji wa Rais wa Burundi, Willy Nyamitwe, alisema amesikitishwa sana na mauaji ya mwanasiasa huyo, ambaye pia ana taaluma ya uandishi wa habari.

“Nimesikitishwa sana, dada yangu mkubwa Hafsa Mossi, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, ameuawa kwa kupigwa risasi na wahalifu. Pumzika kwa Amani,” aliandika kwenye akaunti yake ya Twitter.

Waziri wa Mambo ya Nje, Alain Aime Nyamitwe, pia ameeleza kusikitishwa kwake na mauaji hayo.

“Nimehuzunishwa na mauaji ya leo dhidi ya Mheshimiwa Hafsa Mossi, na mbunge wa EALA. Ni hasara kuu kwa taifa na EAC kwa ujumla,” aliandika katika akaunti yake ya Twitter.

Mauaji ya Mosi ambaye alikuwa mwenyekiti wa wabunge wa Burundi wa EALA, yamekuja huku kukiwa na mlolongo wa mashambulizi dhidi ya maofisa wa juu serikalini yanayofanywa na makundi yasiyojulikana.

Tangu mgogoro uanze mwaka jana watu zaidi ya 500 wameuawa na maelfu kuikimbia nchi baada ya kuibuka upinzani kupinga hatua ya Rais Pierre Nkurunziza kuwania urais kwa muhula wa pili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles