28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mbowe, Zitto waangukiana

Zitto-Kabwe-na-Mbowe-Feb-3-2016*waahidi kuzika tofauti zao

Na Elizabeth Hombo, Dar es Salaam

UHASAMA uliodumu kwa muda mrefu kati ya Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo) na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe sasa ni wazi unaonekana kumalizika.

Hali hiyo inatokana na viongozi hao kwa nyakati tofauti jana kuweka ujumbe kwenye mitandao yao ya kijamii ya facebook na twiter, ambao unaonyesha kila mmoja akijutia makosa yake na kutaka waungane kwa ajili ya kutetea masilahi ya taifa.

Tangu kuanza kwa mijadala mbalimbali bungeni mjini Dodoma wiki iliyopita, Mbowe na Zitto wameonyesha kukubaliana katika misimamo yao na hivyo kuzua maswali kwamba huenda mbunge huyo wa Kigoma Mjini anataka kujiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Mbowe ambaye pia ni kiongozi wa kambi ya upinzani bungeni, akiwa na Zitto wiki iliyopita waliwaongoza wabunge wengine wa Ukawa kususia kikao cha Bunge kupinga hatua ya Serikali kusitisha matangazo ya moja kwa moja ya Bunge kupitia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).

Baadaye viongozi hao pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR Mageuzi, James Mbatia, waliitisha mkutano na waandishi wa habari kueleza umma ambavyo Serikali inarudisha taifa katika zama za udikteta kwa kuzuia haki ya wananchi kupata habari.

Katika kikao hicho cha Bunge, Serikali kupitia kwa Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye, ilitoa taarifa kuwa wanasitisha matangazo hayo ya moja kwa moja ili kubana matumizi ya Serikali yanayofikia zaidi ya Sh bilioni nne kwa mwaka.

 

Katika ukurasa wake wa facebook na twitter jana, Zitto alinukuu ujumbe wa Mbowe uliotoka katika gazeti la kila siku (si MTANZANIA) ambao ulitafsiriwa kwamba ni hatua ya kiongozi huyo wa upinzani kutaka kumaliza tofauti zake za kisiasa na mbunge huyo.

“Kushirikiana na Zitto si jambo la ajabu kama ambavyo umeona tukifanya. Yapo majeraha mengi ambayo tumeyapitia pande zote (Chadema na Zitto) ambayo huwezi kuyatibu kwa siku moja. Yapo ambayo yatapona kulingana na muda. Unaweza kumfanyia mtu kitu kibaya, lakini baadaye ukatambua kuwa umekosea. Chochote katika siasa kinawezekana,” aliandika Mbowe.

Jana kupitia ukurasa wake wa facebook, Zitto ambaye pia ni Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, alisema nafasi ya chama chake bungeni ni upande wa upinzani hivyo atakuwa pamoja na Ukawa.

“Mbowe siku zote amekuwa kiongozi wangu na siwezi kubeza nafasi yake katika kujenga demokrasia nchini. Tulipishana, tulikoseana, tusameheane.

“Mimi binafsi siwezi kuwa mfungwa wa magomvi yetu ya miaka ya nyuma. Nilishasamehe walionikosea na kuomba radhi niliowakosea.

“Tunaweza kupishana kwenye mkakati wa utekelezaji, hatuwezi kupishana kwenye masilahi ya nchi yetu ya kujenga demokrasia na kukataa udikteta.

“Nafasi ya ACT-Wazalendo bungeni ni upande wa upinzani, na hivyo tutakuwa na wenzetu wa upinzani kwenye kujenga hoja zote za kitaifa.

“Mimi nikiwa mbunge wa ACT-Wazalendo, natekeleza kwa vitendo maelekezo ya chama kwa kushirikiana na wabunge wenzangu wa upinzani bungeni.

“Chama chochote makini huweka tofauti binafsi pembeni kwa masilahi mapana ya taifa. Chama cha ACT-Wazalendo kinaamini katika umoja,” alisema Zitto.

Zitto alifukuzwa Chadema na kujiunga na ACT-Wazalendo Machi 21, 2015 chama ambacho hakina ushirikiano na vyama vinavyounda Ukawa, lakini ameonekana kuwa karibu na umoja huo katika vikao vya Bunge la 11 vinavyoendelea mjini Dodoma.

Mwaka 2013, mwanasiasa huyo machachari pamoja na aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu Chadema, Profesa Kitila Mkumbo na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba walifukuzwa kwenye chama hicho, baada ya mfulululizo wa muda mrefu wa mivutano ya uongozi na baadaye wakaanzisha chama cha Alliance for Change and Transparency (ACT) mwaka 2014.

Chadema ilichukua uamuzi huo baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kutupilia mbali pingamizi la Zitto dhidi ya Kamati Kuu kutojadili uanachama wake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles