24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MBARAWA APANGUA HOJA ZA WABUNGE RELI, BOMBARDIER

NA GABRIEL MUSHI, DODOMA


BAADA ya siku tatu za wabunge kuichambua hotuba ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, huku wengi wakijielekeza kwenye gharama za mradi wa ujenzi reli ya kisasa ya Standard Gauge, na ununuzi wa ndege za Serikali, waziri mwenye dhamana na sekta hiyo, Profesa Makame Mbarawa, amejibu hoja zao huku akisema Serikali haitoacha kununua ndege.

Akijibu hoja zilizotolewa na wabunge tangu Jumatatu, Profesa Mbarawa alisema kwa sasa mbali na ndege tatu ambazo zinasubiriwa, Serikali inatarajia kununua ndege nyingine kubwa ya masafa marefu na kufanya idadi ya ndege zinazotarajiwa kununuliwa kuwa saba, tatu zikiwa zimeshawasili nchini.

Alisema Serikali haikurupuki kununua ndege hizo  kwa kuwa inao mpangokazi unaobadilishwa kila mara kulingana na wakati.

Profesa Mbarawa alitoa kauli hiyo bungeni mjini Dodoma ambapo pamoja na mambo mengine alisema Serikali itaendelea kununua ndege na haitokodi kwa sababu kukodi ni gharama kubwa ikilinganishwa na kununua.

“Nia ya serikali ni nzuri kwani huwezi kuwa na viwanja vya ndege kama huna shirika lako la ndege, hivyo tumenunua ndege sita ambazo tatu zimetua na zinafanya kazi. Mwaka huu tunategemea  ndege tatu zitawasili ambazo ni Boeng 787 ya masafa marefu yenye uwezo wa kuchukua abiria 262, nyingine mbili zenye uwezo wa kuchukua abiria 132 kila moja ni Bombardier CHCS 300 ambazo zitawasilia na kuanza kufanya kazi.

“Kikawaida huwezi kuwa na ndege moja ya masafa marefu ikafanya kazi vizuri, hivyo kwenye bajeti hii tumeshapanga kununua ndege nyingine boeng 787 ili tuwe na ndege mbili za masafa marefu ambapo moja ikiwa inatoka Dar es Salaam kwenda Guangzhou na moja inatoka Guangzhou kuja Dar es Salaam. Ndio utaratibu unavyokwenda,” alisema.

Aidha, alisema kampuni ya ndege ya Tanzania inao mpango kazi hivyo si kweli kwamba haina kama wabunge walivyodai.

“Niwahakikishie wabunge na Watanzania tunayo-business plan, na kila baada muda inabadilishwa sio msaafu hivyo itabadilishwa kutokana na mahitaji ya soko,” alisema.

Hata hivyo, alisema Serikali itaendelea kununua ndege mpya ni na haitokodi kama baadhi ya wabunge walivyotaka.

“Makampuni mengi ya ndege kama vile ya Kenya Air ways, Rwanda Airways na Ethiopia wananunua. Wanakodi kama kumetokea route mpya ya haraka. Ukinunua ndege mpya discount (punguzo) kubwa inakupa faida kwenye uendeshaji wako.

“Mfano kuna njia mbili za kukodi ndege ambapo ya kwanza unakodi bila marubani au unakodi na marubani na njia rahisi ni kukodi bila marubani.

“Kwa hiyo bei ya wastani kukodi ndege kwa mwezi ni dola 200,000 hadi 250,000 kwa mwezi, gharama ya matengenezo 18,000, ukikodi ndege unatakiwa kulipa kodi ya dola  za Marekani 25,000   jumla kwa mwezi mmoja unatakiwa angalau uwe na dola 300,000 kwa mwaka uwe na dola milioni 3.5 ukikodi ndege ukichimua na bima milioni kwa mwaka.

“Sasa ndege za mpya zinaishi kwa muda miaka 35. Sasa ukiendelea kukodi ndege kwa muda wa miaka hiyo 35 utatumia Dola za Marekani milioni 140. Lakini sisi tutanunua ndege mpya kwa Dola za Marekani milioni 35 kukodi ndege ni gharama kubwa kuliko kuinunua. Watanzania wamenisikia,” alisema.

Aidha, alisema mpaka mwisho wa mwaka huu ATCL litakuwa limeingizwa kwenye mfumo wa anga wa kimataifa IATA.

Alisema shirika hilo liliondolewa kwenye mfumo huo tangu mwaka 2008 kutokana na madeni

Hata hivyo, alisema kuhusu hesabu za ATCL kutowasilishwa bungeni, hesabu hizo hazijawasilishwa kwa sababu shirika hilo halijakaguliwa kuyanzia mwaka 2007 hadi 2015.

“Serikali tulimwagiza CAG akague kuanzia mwaka 2007 hadi 2015,  na kazi imekalimika ripoti imepelekwa kwenye bodi ya ATCL, kazi inayofuata sasa ni ukaguzi wa 2016/17, nia ni kuhakikisha ATCL inasisima na tukiweka Sh tano inatumika kwa masilahi ya watanzania hivyo tumejipanga.

 

Kwa habari zaidi jipatie nakala ya gazeti la MTANZANIA.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles