Na MWANDISHI WETU-DAR ES DALAAM
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amezindua bodi ya Ushauri ya Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI) na kuwataka viongozi hao kuwawezesha vijana kushika nafasi mbalimbali zikiwamo za unahodha.
Alisema ni vema kufanya hivyo kwa sababu kwa sasa nafasi nyingi zimeshikwa na wazee.
Profesa Mbarawa alisema a kama taifa huo siyo mwelekeo mzuri huku akiwasisitiza wajumbe wa bodi hiyo kufanya kazi kwa uadilifu na uwazi kuiendeleza nchi.
Akizindua bodi hiyo Dar es Salaam jana, Waziri Mbarawa alisema wajumbe wapya wa bodi hiyo wanayo nafasi ya kukipeleka chuo mbele.
Aliwashukuru wajumbe waliomaliza muda wao kwa kazi nzuri waliyoifanya.
Waziri alisema taasisi hiyo ina wajibu wa kufundisha vijana ambao watalitumikia taifa wakiwa na umri mdogo badala ya hivi sasa ambako nafasi nyingi kama za unahodha na uhandisi zimeshikwa na watu wenye umri mkubwa.
“Nalizungumza hapa msaidie kuelewa kwamba kama taasisi mna wajibu wa kuwawezesha vijana kushika nafasi mbalimbali kama unahodha na nyinginezo kwa vile kwa sasa nafasi nyingi zimeshikwa na wazee kama taifa huo siyo mwelekeo mzuri,” alisema na kuongeza:
“Natoa ushauri huu si kama Waziri tu….la hasha pia kama mdau wa sekta hii kwa sababu nimejihushisha na shughuli za usafiri wa meli kwa muda mrefu sasa, nina ifahamu vema sekta hii”.
Waziri alisema anatambua chuo hicho kinakabiliwa na uhaba wa miundombinu ya kufundishia, majengo na ufinyu wa bajeti ya mafunzo, hivyo atashirikiana na Bodi ya Chuo hicho kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo.
“Nitashirikiana na bodi yenu, ikiongozwa na Nahodha mzoefu, Bupamba na ni matumaini yangu kwamba kwa pamoja tutaweza kukabiliana nazo.
Alisisitiza kwamba serikali ina wajibu wa kuhakikisha taasisi zilizo chini yake zinafanikiwa katika kukabiliana na changamoto na hivyo kutoa huduma bora kwa wananchi.
Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Nahodha Bupamba alimhakikishia Waziri kwamba taasisi yake itashirikiana na serikali kuhakikisha malengo ya chuo hicho yanafikiwa.
“Nakushukuru Mheshimiwa Waziri kwa kufika, na pia kwa imani ambayo Mheshimiwa Rais ameionyesha kwangu kwa kuniteua,” alisema.
Bodi hiyo ina wajumbe watano ambao mbali na Mwenyekiti, Nahodha Ernest Bupamba, wengine ni Dk.Mwamini Tulli, Tumaini Silaa, Alfred Misana na Andre Matillya.
Mkuu wa Chuo hicho, Dk. Erick Massami alisema taasisi hiyo imeendelea kukua mwaka hadi mwaka ikiwa inatoa kozi mbalimbali kwa viwango vya cheti hadi shahada.