26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MAZINGIRA MABAYA SHULENI YAKIMBIZA WALIMU, WANAFUNZI KUFELI

Na Ramadhan Libenanga, Morogoro


WanafunziSHULE za msingi mkoani Morogoro zimekuwa  zikikabiliwa na changamoto  nyingi.

Miongoni mwa changamoto hizo ni uchakavu  wa majengo, uhaba wa nyumba za walimu, ukosefu wa vyoo vya wanafunzi  na uhaba wa walimu shuleni.

Changamoto hizo ni miongoni mwa mambo yanayochangia wanafunzi mkoani Morogoro kufanya viabaya katika mitihani yao ya mwisho.

Wilaya za Mvomero, Kilosa na Morogoro Vijijini zinatajwa kufanya vibaya katika matokeo ya darasa la saba mwaka jana. Chanzo cha matokeo hayo kuwa mabaya inasemekana kuwa ni mazingira mabovu ya shule  nyingi zilizopo wilayani humo.

Wilaya ya Morogoro Vijijini  inatajwa kushika mkia katika  matokeo hayo ya darasa la saba.

Idadi ya shule zilizofanya vibaya ni 13 ambazo zinatoka katika tarafa za Bungu, Kilole na  Kisanga.

Mratibu wa Elimu Tarafa ya  Kasanga, Innocent Mloka anasema mazingira  ya shule nyingi ni mabaya hivyo wanafunzi wengi hushawishika kutoroka shuleni kabla ya muda wa masomo kuisha.

“Shule nyingi hazina vyoo hivyo walimu hulazimika kuwaruhusu  wanafunzi kwenda nyumbani  kujisaidia, jambo ambalo huwafanya wengi wao wasirudi darasani pindi wanapokwenda nyumbani,” anasema.

Anasema kuwa mazingira  mabaya ya miundombinu  kuanzia barabara, madarasa na  nyumba za walimu pia umekuwa ukichangia utoro kwa wanafunzi.

“Uhaba wa walimu nalo ni tatizo kubwa kwani kutokana na kuelemewa na masomo, hujikuta wakishindwa kumaliza silabasi  kwa wakati na hivyo wanafunzi kujikuta wakikosa maswali mwengi katika mitihani yao ya mwisho.

“Katika shule zetu zote walimu  na wanafunzi bado wanajisaidia  vichakani, mazingira ya  darasani nayo mabaya, nyumbani  pia ni shida tupu hivyo walimu wengi hawapendi kufundisha huku,” anasema mratibu huyo.

Naye Mratibu wa Elimu Tarafa  ya Kolelo, Salim Timbushe anasema kuwa walimu wengi  hukataa kufundisha katika shule  za pembezoni kutokana na mazingira ya kufundishia kuwa mabaya.

Kwa upande wao baadhi ya wazazi wa wanafunzi hao wanasema kuwa katika maeneo wanayoishi mwamko wa elimu  bado ni mdogo.

Kwamba wazazi wengi wanaona  ni vema watoto wao wakatufute riziki mitaani badala ya kwenda shuleni.

“Watoto wengi wakitoka shule wanakimbilia kwenda kuuza bidhaa mitaani na wengine kuendesha bodaboda, kubeba  mizigo kwa waachuzi wa mazao, na kwenda migodini badala  ya kujisomea,” anasema Khadija  Masoud.

Anasema kwa hali hiyo utagundua kuwa wazazi  nao ni kikwazo, badala ya kuwahimiza watoto kujisomea, wanawaacha waende mitaani kutafuta fedha… hii yote ni kutokana na hali ngumu ya maisha inayowakabili.

“Shuleni nako ni shida, sijui huwa wanafundishwa nini hawa watoto wetu. Mimi huwa nina desturi ya kuchunguza madaftari ya mwanangu, lakini tangu aanze shule huu mwaka  wa tatu sijawahi kuona daftari lake hata moja likiwa limejaa,” anasema mmoja wa wazazi aliyejitambulisha kwa jina Zamoyoni Juhudi.

Akizungumzia suala hilo, Ofisa Elimu Mkoa wa Morogoro, Wariambora Nkya anakiri kuwapo kwa  changamoto hizo na kwamba wanajitahidi kukabiliana nazo.

Anasema kuwa shule nyingi ni chakavu na kwamba utaratibu  wa kuzifanyia ukarabati unaendelea kufanyika mwaka   hadi mwaka.

Anasema kuwa wanashindwa kumaliza tatizo hilo kwa wakati kutokana na wingi wake.

Kuhusu suala la walimu kukataa  kufundisha shule zilizopo katika  mazingira magumu, anasema kuwa ofisi yake kwa kushirikiana na halmashauri inaendelea  kutafuta njia za kuwashawishi  walimu kwenda katika shule hizo.

“Kuhusu suala la vyoo tunawaomba  wazazi  washirikiane na  halmashauri kujenga vyoo bora shuleni ili kuepusha wanafunzi kupata magonjwa ya mlipuko,” anasema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles