29.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Maximo basi tena Yanga

Kocha-wa-Timu-ya-Club-ya-Yanga-Maxio-MaximoNA MWANDISHI WETU, DAR ES SAALAM,

UONGOZI wa klabu ya Yanga umeamua kukatisha mkataba wake na kocha wa timu hiyo, Mbrazil Marcio Maximo kuanzia sasa ukiwa ni uamuzi ulioafikiwa katika kikao kilichofanyika juzi Hoteli ya Protea, jijini Dar es Salaam.
Kikao hicho kimekaa siku moja baada ya timu hiyo kuchapwa bao 2-0 na watani wao wa jadi, Simba katika mchezo wa Nani Mtani Jembe uliofanyika mwishoni mwa wiki Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Maximo anaondolewa katika kikosi hicho akiwa ameshiriki katika mechi tisa tu za timu hiyo, ikiwa ile ya Ngao ya Hisani dhidi ya Azam, mechi saba za Ligi Kuu Tanzania Bara na hii ya juzi ya Mtani Jembe.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Yanga zililipasha MTANZANIA kuwa, kikao hicho kiliamua taratibu za kuondolewa kwa kocha huyo zianze mara moja, huku kikitaja sababu kubwa za kuondolewa Maximo ni kutumia mfumo wa zamani kufundishia timu hiyo ambao hauendani na soka la sasa.
Mpasha habari huyo alisema, mbali na uamuzi wa kuondolewa kwa Maximo, mchezaji Andrew Coutinho ataondolewa pia na nafasi yake kuchukuliwa na Hamis Kiiza ambaye tayari uongozi ulipanga kumtema.
“Viongozi walikutana juzi na uamuzi ulioamuliwa ni huo, kwanza mchakato wa kuvunjwa kwa mkataba na Maximo na Counthio uanze mara moja.
“Maximo ni kocha mzuri sana hata ubora unajulikana, lakini ameshindwa kuisaidia timu kwa kutumia mifumo yake ya kizamani kuendesha timu,” kilisema chanzo hicho.
Hata hivyo, inaelezwa tayari Kocha huyo aliyesaini mkataba wa miaka miwili mwezi Juni mwaka huu kuitumikia klabu hiyo, ameshalipwa stahiki zake.

Wakati huo huo Kocha kipenzi wa Yanga, Hans van der Pluijm, aliyewahi kuinoa timu hiyo mzunguko wa pili wa msimu uliopita, anatua nchini leo mchana kufanya mazungumzo na uongozi wa timu hiyo kwa ajili ya kurejea katika wadhifa wake.
Mholanzi huyo aliyemaliza mkataba wa kuinoa Yanga msimu uliyopita, aliondoka nchini na kwenda Uarabuni alikopata ofa ya kuinoa klabu ya huko ambayo hata hivyo alishindwa kuendelea nayo baada ya kutofautiana na viongozi.
Kufuatia taarifa hizo tata za kuja Pluijm, MTANZANIA liliwasiliana na Boniface Mkwassa, ambaye alishindwa kuweka wazi kama yupo tayari kuinoa Yanga na badala yake kuwatupia mpira viongozi wa klabu hiyo.
“Siwezi kuzungumza chochote kuhusu suala hili la mimi kuifundisha Yanga, nawaachia viongozi ndiyo wenye dhamana ya kutoa taarifa kamili,” alisema Mkwassa.
Kwa takribani mwezi mmoja sasa tangu kusimama kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, Mkwassa amekuwa akitajwa kurejeshwa Yanga kutokana na kile kinachoelezwa klabu hiyo kutoridhishwa na kiwango cha timu yao.

Mkwassa aliwahi kuinoa Yanga akiwa kama msaidizi wa Pluijm, ambaye baada ya kumalizika kwa mkataba wake wa miezi sita alitimkia Uarabuni akiwa na Kocha huyo mzalendo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles