24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Matukio ya utekaji yaliyoishangaza dunia

TUKIO la kutekwa kwa mfanyabiashara maarufu nchini, Mohamed Dewji limewashangaza wengi, huku polisi wakiendelea kumtafuta.

Katika historia, yapo matukio ya watu wengi maarufu kutekwa na hata kuushangaza ulimwengu. Hapa, tunakusimulia kumi yanayoshangaza zaidi.

JOHN PAUL GETTY III

Tukio hili linakumbukwa na wengi baadhi wakidai ni mfano wa madhara ya mtu kuwa bahili. Mwaka 1973, wahalifu walimteka mjukuu wa tajiri wa mafuta Jean Paul Getty, aliyefahamika kwa jina John Paul Getty III ambaye alikuwa na miaka 16 wakati huo.

Alitekwa akiwa katika jumba la Piazza Farnese jijini Roma, Italia. Watekaji walitaka kulipwa dola milioni 17 ambazo ukilinganisha na utajiri wa babu yake, zilikuwa pesa kidogo. Lakini mzee huyo mpango wake ulikuwa tofauti.

Isitoshe, mjukuu huyo alikuwa mtukutu na mara kadha alikuwa anawatania watu kwamba anaweza hata kujiteka nyara. Alipopewa ujumbe wa madai ya watekaji, babu yake aliupuuza.

Isitoshe, aliamini kwamba kama angelipa pesa hizo basi angewaweka hatarini jamaa zake wengine kwa watekaji kuwalenga na kudai fedha. Akaamua kutolipa chochote.

Watekaji walipoona wataondoka mikono mitupu, waliamua kumtumia ujumbe. Walimkata mvulana huyo sikio na kutuma kipande chake pamoja na fungu la nywele kwa gazeti moja, na ujumbe unaosomeka kwamba iwapo pesa hazingelipwa, wangekuwa wakikata kipande kila wakati na kutuma hadi walipwe pesa hizo.

Maskini wa watu alilazimika kulipa na mvulana huyo akarejeshwa, lakini tukio hilo liliathiri sana maisha yake. Kufikia wakati wa kulipa, watekaji walikuwa wamepunguza kiasi cha fedha hadi dola milioni 3, ambazo ndizo zilizolipwa.

Babu huyo alilipa dola milioni 2.2 mwenyewe – kiasi cha juu zaidi ambacho aligundua kwamba angelipa bila kutozwa kodi. Kiasi kilichosalia kikilipwa na mwanawe (babake mtoto).

IVAN KASPERSKY

Iwapo unafahamu mambo ya kompyuta na mitandao, basi itakuwa ajabu iwapo jina la Kaspersky haujawahi kulisikia.

Kaspersky ni mtoto wa Eugene Kaspersky tajiri mtengenezaji wa programu za kompyuta na programu za kupambana na virusi vya kompyuta na pia wadukuzi.

Mwaka 2011, genge la watekaji  lilifanikiwa kumteka mtoto wake aliyekuwa na umri wa miaka 20 wakati huo. Alizuiliwa mjini Moscow na watekaji wakaitisha kikombozi.

Lakini walifanya makosa yaliyowasaidia wapelelezi kujua walikuwa wanamzuilia wapi. Polisi walifuatilia mawimbi ya moja ya simu waliyotumia kumpigia baba yake kijana huyo wakidai fedha.

Kwa mujibu wa jarida la Forbes, utajiri wa Eugene Kaspersky unakadiriwa kuwa dola bilioni 1.4, karibia sawa na Mohammed Dewji. Ana watoto wanne.

PATTY HEARST

 

Patty Hearst ni mjukuu wa tajiri mmiliki wa kampuni ya uchapishaji magazeti William Randolph Hearst. Umaarufu wake ulimweka hatarini.

Mwaka 1974, akiwa na miaka 19 alishambuliwa, hadi akapoteza fahamu na kutekwa nyumbani kwake California.

Kundi la siasa za mlengo wa kushoto kwa jina SLA, ambalo lilikuwa linaelekezwa na Profesa wa Chuo Kikuu cha California, lilidai kuhusika.

Sharti lao lilikuwa kwamba familia ya Hearst itoe chakula cha thamani ya dola 70 kwa kila familia maskini jimbo la California jumla dola milioni 400.

Baba yake Patty alichukua mkopo na akapanga kutoa chakula cha thamani ya dola milioni 2 ambacho kiliangushwa katika eneo la Bay Area kwa ajili ya kutumiwa na jamii maskini.

Hilo halikuwaridhisha watekaji. Ili kujiokoa, Patty alilazimika mwenyewe kukubali kuwa mwanachama cha SLA na baadaye akashiriki shughuli zao ambapo miongoni mwa mengine walitekeleza wizi. Mwishowe alikamatwa na kufungwa jela miaka 35 kwa kosa la wizi wa benki.

WALTER KWOK

Mwaka 1990, Walter Kwok na ndugu zake wawili walirithi mali ya kampuni tajiri zaidi katika biashara ya ardhi na majumba jijini Hong Kong, Sun Hung Kai Properties pamoja na mali ya baba yao Kwok Tak Seng.

Mara moja, wakawa kwenye orodha ya Forbes ya watu tajiri zaidi duniani. Wapenda vya bure wakawa wanamezea mate utajiri wao.

Mwaka 1997 Kwok alitekwa na jambazi maarufu Cheung Tze-keung, maarufu zaidi kwa jina ‘Big Spender’. Mke wake Kwok, Wendy alifanikiwa kushauriana nao na kufanikisha uhuru wake bila kuwashirikisha polisi.

Ingawa hakukuwa na taarifa yoyote rasmi kuhusu kiasi cha fedha kilicholipwa na kumkomboa, Tze-keung alidai alilipwa dola milioni 600 kumwachilia Kwok. Alikamatwa baadaye kwa makosa mbalimbali, na akauawa nchini China disemba 16, 1998 baada ya kuhukumiwa kifo.

ALDO MORO

Aldo Moro alikuwa mwanasiasa maarufu nchini Italia aliyependwa sana na raia. Alikuwa amehudumu kama Waziri Mkuu kati ya 1963-1968.

Moro alikuwa ndiye waziri mkuu aliyekuwa amehudumu muda mrefu zaidi tangu wakati wa vita vikuu vya dunia. Lakini umaarufu wake na kupendwa kwake na watu pengine vilimharibia mambo.

Machi 1978, wanachama wa kundi la wanamgambo wa Red Brigades, waliwaua walinzi wake watano na kumteka kutoka kwenye barabara moja Roma.

Waliitisha kuachiliwa huru kwa wenzao 16 waliokuwa wanazuiliwa na serikali ndipo waruhusu kumwachilia huyu Moro. Serikali ilikataa.

Alipigwa risasi mara kumi akiwa kwenye gari na kuachwa akiwa marehemu baada ya kuzuiliwa kwa siku 55.

FRANK SINATRA JR

Mwana wa mwanamuziki maarufu Frank Sinatra na mkewe Nancy, Frank alikuwa na miaka 19 alipotekwa 1968. Kijana huyo alitekwa na wanaume watatu Barry Keenan, Johnny Irwin na Joe Amster, kwenye chumba nambari 417 katika hoteli ya Harrah ufuo wa Ziwa Tahoe.

Baba yake Frank Sr alilipa dola 240,000. Baada ya kuzuiliwa kwa siku mbili, aliachiliwa huru.  Tukio hilo lilizua utata, baadhi wakifikiri pengine mwanamuziki huyo alikuwa anajitafutia njia ya kufufua umaarufu wake, siku hizi utasema pengine alikuwa ‘anajitafutia kiki’.

Wahusika, wanaume hao watatu walikamatwa baadaye na kupatikana na hatia, ingawa aliyepanga utekaji nyara huo, Keenan, baadaye alitangazwa kisheria kuwa mwenye matatizo ya akili.

CHARLES LINDBERGH JR.

Lilikuwa tukio lililoishangaza na kuisikitisha dunia mwaka 1932. Charles Lindbergh Jr alikuwa mwana wa rubani maarufu wa ndege Charles Lindbergh ambaye alikuwa pia mwandishi maarufu.

Alikuwa anatazamwa na wengi kama ‘Shujaa wa Marekani’ baada ya kuwa wa kwanza kufanikiwa kuvuka bahari ya Atlantiki akiwa kwenye ndege peke yake.

Mtoto huyo alikuwa na miezi 20 alipotekwa nyumbani kwao New Jersey. Mtekaji aliacha ujumbe uliokuwa na makosa mengi ya kisarufi, akidai dola 50,000, na hata kueleza alipwe kwa sarafu za thamani gani.

Alitahadharisha pia dhidi ya kutangazwa kwa tukio na kuhusishwa kwa polisi. Hata hivyo taarifa zilienea haraka. Licha ya hakikisha kwamba mtoto wao angekuwa salama baada ya kulipa fedha zilizotakiwa na mtakeji, mwili wa mtoto huyo ulipatikana vichakani miezi miwili baada ya kutekwa.

Polisi walifanikiwa kumtafuta mtekaji kwa kufuata nambari za usajili za dola zilizotumiwa kulipa madai yake.

Richard Hauptmann alikamatwa na kupatikana na hatia ya utekaji nyara na mauaji. Aliuawa 1936 kwa umeme.

FAMILIA YA JENNIFER HUDSON

Jennifer Hudson alipata umaarufu aliposhiriki katika kipindi cha American Idol mwaka 2004. Ingawa alimaliza akiwa wa saba, nyota huyo alipata umaarufu kutokana na kipaji chake.

Mwaka 2008, alipata pigo kubwa pale mama yake wa miaka 57 Darnell, ndugu yake Jason, 29, na binamu yake Julian, 7, walipozuiliwa mateka na kisha kuuawa kwa kupigwa risasi.

Mshambuliaji alikuwa anawafahamu vyema. William Belfour alikuwa mume wa zamani wa dada yake. Alikamatwa na kushtakiwa na akahukumiwa vifungo vitatu vya maisha na miaka mingine 120.

BBC

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles