MEYA wa Jiji la Mbeya, David Mwashilindi, ameahidi kusimamia na kushughulikia tatizo la baadhi ya vijana walioathirika na dawa za kulevya ili nguvu kazi ya taifa isizidi kupotea.
Meya Mwashilindi aliyasema hayo jana baada ya kupokea maombi ya vijana zaidi ya 40 wa jijini Mbeya, ambao wameiomba Serikali na wadau wengine kuwasaidia matibabu ili waachana na matumizi hayo ya dawa.
Pia vijana hao maarufu ‘mateja’ wameomba kupatiwa shughuli ya kufanya ili waondokane na vitendo vya uhalifu ambavyo asilimia kubwa vinawasababishia kupigwa au kuuliwa na wananchi wenye hasira.
Vijana hao walimuahidi Meya wa Jiji hilo kubadilika na kuachana na matumizi ya dawa hizo, kwani zimekuwa zikihatarisha uhai wao kwa kiasi kikubwa.
Akitoa ombi hilo jana, Mwenyekiti wa vijana hao ambao shughuli yao kuu ni kupiga debe katika stendi kuu jijini Mbeya, Shaban Shibu, alisema wamefika mahala na kuona kwamba dawa hizo haziwasaidii kitu chochote zaidi ya kuhatarisha uhai wao.
“Baadhi yetu wamekuwa wakinunua mipigo hadi ya shilingi 50,000 kwa siku, sasa jiulize huyu mtu fedha hiyo anaipata wapi na kazi yake ni upigaji debe, ni lazima ajiingize kwenye vitendo vya uhalifu kwa kuwaibia wasafiri,” alisema Rashid Yasin, Katibu wa kikundi hicho.
Alisema wanachotamani vijana hao ni kurejea katika hali yao ya zamani lakini kwa sasa wanashindwa kutokana na dawa hizo kuwaathiri kwa kiasi kikubwa, hivyo wanaiomba Serikali kuwasaidia kupata matibabu.
“Kati yetu sisi wapo waliotelekeza familia zao, waliofukuzwa na wazazi nyumbani, walioathirika na ugonjwa wa ukimwi pamoja na wale ambao kwa sasa hawajitambui kabisa kutokana na kuathiriwa kwa kiasi kikubwa na dawa hizo,” alisema.
Hata hivyo, Meya Mwashilindi aliwataka vijana hao kuendelea kujitafutia kipato kwa kufanya kazi halali badala ya uhalifu, huku suala lao likiwa linashughulikiwa kwani Mbeya bila uhalifu inawezekana.
Alisema licha ya kusimamia na kushughulikia masuala ya maendeleo, pia tatizo la dawa za kulevya mkoani Mbeya ni kubwa, hivyo yeye binafsi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali atahakikisha suala hilo linatatuliwa ili kuokoa uhai wa maisha ya vijana hao ambao ni nguvu kazi ya taifa.
anza kukimbilia mkoani Songwe baada ya kufukuzwa Chunya.