25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Marufuku maegesho yasiyo rasmi ya magari ya abiria

Na Samwel Mwanga, Maswa

Serikali wilayani Maswa mkoani Simiyu imepiga marufuku uegeshaji wa magari madogo ya abiria katika mitaa mbalimbali mjini Maswa na kuyataka magari yote yanafanya biashara hiyo yaegeshwe kwenye kituo kikuu cha Mabasi na vituo vidogo vilivyowekwa viwili vilivyo rasmi.

Kauli hiyo imetolewa leo Jumatano, Desemba 16, na Mkuu wa wilaya ya Maswa, Aswege Kaminyoge wakati akizungumza na wadau wa usafirishaji katika wilaya hiyo.

Amesem Halmashauri ya wilaya hiyo ilijenga kituo hicho chenye nafasi kubwa kwa ajili ya mabasi na magari yote yanayofanya biashara ya kusafirisha abiria lakini anashangaa kuona bado baadhi ya magari yanaegeshwa katika vichochoro vilivyoko mjini humo.

“Tumejenga kituo kikuu cha mabasi mjini Maswa na hii inatumika kwa magari yote ya abiria yale makubwa yaani Mabasi na yale magari madogo madogo ambayo mengi yao yanakwenda maeneo ya vijijini wapo wanaokuja kuegesha katika kituo hicho lakini yapo mengine yanaegeshwa kwenye mitaa tena uchochoroni suala hili halikubaliki,”amesema Kaminyonge.

Amesema uegeshaji huo usiyo rasmi umekuwa ukiisababishia hasara halmashauri hiyo kutokana na malengo yake ya kukusanya ushuru na hivyo kuifanya ishindwe kufikia malengo yake ya kuwahudumia wananchi kupitia mipango waliyojiwekea.

“Suala hili limekuwa kero sasa katika mji wa Maswa naagiza wote wanaohusika kulishughulikia suala hili na jeshi la polisi mhakikishe
kuwa maegesho yote yasiyo rasmi ya vituo vya abiria visiwepo mara moja maana tumeshuhudia ajali zilizopoteza maisha ya watu kutokana na
kuwepo kwa maegesho hayo hivyo kamateni magari yote hayo na watozeni faini na wakizidi wafikisheni mahakamani,”amesema.

Pia ametumia muda huo kutoa wito kwa madereva wa magari hayo kuwa ni vema wakaheshimu sheria na taratibu zilizopo zinazowataka kuegesha
magari yao katika maeneo yaliyotengwa na halmashauri ili kuepusha kutolipa mapato ya serikali.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Barabarani wilaya ya Maswa, Samwel Mwanga amesema kuwa Sheria ya Mipango miji inatoa muongozo ya kupanga mji na sio kufanya shughuli zao na kukaa kiholela holea hata katika maeneo hawakupangiwa kuegesha.

Amesema kwa sasa watafanya zoezi kimya kimya ili kuwabaini madereva wote wanaokiuka sheria zote za usalama barabarani ambao ndiyo
wamekuwa chanzo cha ajali katika wilaya hiyo ili waweze kuchukuliwa hatua za kisheria wakiwemo hao wanaogesha magari yao kwenye maegesho yasiyo rasmi.

“Hapa ni mjini ni lazima madereva waheshimu Sheria ya Mipango miji kwa kuegesha magari yao katika maeneo waliotengewa wakati wanasubiria abiria wao kwa ajili ya kuwasafirisha kwenda maeneo wanayotoa huduma za usafiri na sisi kamati ya usalama barabarani tutafanya kazi yetu ya kuwabaini madereva wanaovunja sheria na taratibu za usalama barabarani,”amesema Mwanga.

 Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Vivian Christian amesema kuwa msimamo wao ni kuwa magari yote yanatakiwa
yaegeshwe katika maeneo maalum yaliyotengwa  kwa ajili ya kupakia na kushusha abiria kinyume cha hapo ni kufanya kosa.

Amesema sheria ya mipango miji, namba 8 ya mwaka 2007 inaongoza ukuaji wa miji na mpangilio wa ukaaji katika mji husika ikiwemo utengaji wa maeneo kwa ajili ya huduma za jamii, biashara , usafari , afya na mambo mengine yanayoufanya mji uonekano nadhifu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles