ADDIS ABABA,Ethiopia
RIPOTI ya awali imewapongeza marubani wa ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopian Airlines ambayo ilianguka na kusababisha vifo vya abiria na wafanyakazi wote waliokuwamo baada ya kuruka muda mfupi kutoka mjini wa Addis Ababa wiki tatu zilizopita.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana mjini hapa, shirika hilo la ndege limemsifia rubani huyo kwa kufuata taratibu zote za tahadhari na dharura kwa kutumia utaalam wake katika mazingira magumu.
Ripoti hyo ya awali inaonyesha kwamba marubani hao wa ndege hiyo namba 302 walifuata maelekezo ya Kampuni ya Boeing na Mamlaka ya Anga ingawa walishindwa kuidhibiti isianguke.
“Tunajivunia marubani wetu kwa kufuata taratibu za dharura na kwa utaalamu wa hali ya juu katika mazingira magumu,”ilieleza sehemu ya ripoti hiyo.
Ripoti hiyo ya awali inafuta madai kwamba marubani hao hawakupata mafunzo mapya jinsi ya kuendesha ndege hiyo aina ya Boeing 737 Max 8, ambayo ilianguka.
Shirika la Ndege la Ethiopia Airline, mara zote limekuwa likiyakana madai hayo na ripoti hiyo inaonekana kupunguza mzigo kwa kampuni ya Boeing ambayo inashutumiwa kwa ndege zake kusababisha ajali, baada ya taarifa za uchunguzi kuonesha kuwa sawa na za ajali ya ndege ya Shirika la Lion Air iliyoanguka Oktoba mwaka jana.
Maelezo ya ripoti ya awali pia yanaonesha kwamba kuna programu ambayo ilijizima na kusababisha ndege kuanguka licha ya ukweli kwamba marubani hao walilazimika kuizima katika harakati zao za kuokoa maisha watu.