25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

MAREKANI KINARA KUWA NA MITAALA BORA CHUO KIKUU

Na FARAJA MASINDE,

LICHA ya mamilioni ya fedha kuwekezwa katika elimu ya juu, hakuna anayetambua thamani yake. Mataifa kama Uingereza, Marekani na mengi yanaamini kuwa jambo la msingi na lenye faida kwa kipindi hiki cha Sayansi na Teknolojia, ni kuwekeza katika  elimu ya juu, jambo ambalo limeyalazimisha mataifa mengine kuiga mfumo huu.

Kuwapo kwa vyuo vikubwa kama Harvard kilichoanzishwa mwaka 1963 na vingine ni moja ya vichocheo vikubwa vilivyoyafanya mataifa mengine kuanzisha utaratibu huu wa kujenga vyuo vikuu.

Watu wengi kutoka mataifa mbalimbali walikuwa wakiwekeza fedha zao hapo kwa ajili ya kuhakikisha wao au kizazi chao kinapata ujuzi wa kutosha.

Kuwa na vyuo imara ndio kumesaidia leo hii nchi ya Marekani kuonekana kuwa na mitaala bora zaidi ya elimu ya juu duniani, jambo ambalo pia limeshawishi mataifa mengine  kuwa na mwamko wa kupeleka wanafunzi wengi huko kutokana na kutambua kuwa ni sehemu nzuri ya kupata elimu ya juu.

Tafiti zilizofanywa kuhusu elimu ya vyuo vikuu duniani na taasisi ya utafiti ya Ujerumani, imebaini kuwa Marekani inaongoza kwa kuwa na mtaala bora duniani kwenye elimu ya juu.

Nchi hiyo imekuwa ikiongoza tangu ilipoanza mwanzoni mwa karne ya 19 na kusambaa kwenye nchi za Ulaya na Asia Mashariki kwenye karne ya 20.

Hadi sasa elimu hii inasambaa kwa kasi kubwa duniani kote ikiwamo barani Afrika.

Kuongezeka kwa vyuo vinavyotoa taaluma hii kumefanya idadi ya wanafunzi kuzidi kupanda na kuongezeka maradufu kutoka asilimia 14 hadi 60 kwa kipindi cha muongo mmoja hadi kufikia 2015.

Utafiti huo unaonyesha kuwa wakati kiwango hicho cha wanafunzi kikiongezeka, idadi ya vyuo kwenye nchi mbalimbali duniani pia imepaa kutoka wastani wa vyuo vitano hadi 54 kwa nchi moja na hivyo kufanya idadi ya vyuo kuongezeka kwa haraka zaidi ikilinganishwa na mahaitaji halisi.

Ongezeko hilo la vyuo limesaidia kutoa mwanya mpana kwa wanafunzi ambao wamekuwa na uhuru wa kuchagua chuo bora zaidi kwa ajili ya kusoma masomo yatakayo wawezesha kufikia ngazi ya shahada ambayo kwa miaka ya karibuni ndio kimekuwa kipimo kikubwa cha elimu na tiketi ya kupata kazi kwa haraka.

Utitiri huu wa vyuo umekuwa ukilazimisha dunia kufuata mwelekeo wa Taifa la Marekani, ambapo vyuo vikuu vingi kwenye mataifa mbalimbali vinalazimika kutoza ada kwa wanafunzi.

Serikali nayo imekuwa ikitoa mikopo kwa wanafunzi wachache, licha ya kutambua kuwa ni jukumu lao kuwasaidia.

Njia hii ya Serikali kubana matumizi imekuwa na faida wakati mwingine.

Mwaka 2000 Marekani ilitumia asilimia 1.6 ya pato lake kugharimia elimu ya juu, jambo ambalo limesaidia nchi hiyo kubana matumizi, kwani kinyume na hapo iliwalazimu kutumia asilimia 2.7 ya pato lake kwa ajili ya elimu ya juu.

Kila mwanafunzi anatamani kusoma hadi ngazi ya shahada ili kupata ajira kiurahisi, lakini baadhi ya ofisi waajiri wamekuwa wakifuatilia zaidi umaarufu na ubora wa chuo husika.

Hii ni kwa sababu baadhi ya vyuo vimekuwa vikijivunia kuzalisha wahitimu wengi lakini hawana ubora wowote.

Barani Asia baadhi ya nchi zinaendelea kuboresha vyuo vyake kwa kile wanachoamini kuwa vikiwa bora watapata wanafunzi wengi wa kimataifa watakaowasaidia kunyanyua kiwango cha elimu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles