30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Marais wa Afrika wenye damu ya muziki

CHRISTOPHER MSEKENA

BILA shaka utakuwa umewahi kushuhudia, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dk John Magufuli, akipiga ala za muziki hasa tumba kwa umahiri mkubwa katika matukio mbalimbali hapa Bongo.

Mfano ni Octoba 21, 2016, katika sherehe za kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa mabweni 20 ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais Magufuli aliungana na wanamuziki wa bendi ya Msondo Ngoma kutumbuiza kibao cha Tanzania Yetu Nchi ya Kupendeza na yeye akiwa kama mpiga tumba aliyenogesha wimbo huo.

Hayo ni mapenzi makubwa aliyonayo Rais wetu kwenye muziki ni sawa kabisa na marais wengine wa Afrika ambao Swaggaz tumewatambua kama wana damu ya muziki kutokana na ushiriki wao katika tasnia hiyo kwenye nchi wanazo au walizowahi ziongoza.

ANDRY RAJOELINA

Huyu ni rais wa sasa wa Madagascar mwenye umri wa miaka 44. Akiwa na miaka 19, Andry alitambua fursa iliyopo kwenye kiwanda cha muziki nchini humo, hivyo akaanzisha kampuni inayoitwa Show Business, iliyokuwa inandaa maonyesho ya burudani.

Mwaka 1994, biashara hiyo ilifanikiwa zaidi kwani Andry  ambaye aliyekuwa mchezesha muziki yaani DJ kwenye maonyesho hayo, aliweza kufanya kazi na wanamuziki mbalimbali wa kisiwa hicho kiasi cha maonyesho yake kuhudhuriwa na mashabiki zaidi ya 50,000 ndani ya miaka 10 toka alipoanza biashara hiyo ya muziki.

2007, Andry alifanikiwa kununua kituo cha runinga na redio alivyovipa jina la Viva ambavyo mpaka sasa licha ya kuripoti matukio mbalimbali ya siasa na kijamii vimeendelea kusapoti sanaa ya Madagascar.

ARMANDO GUEBUZA

Huyu ni rais wa zamani za Msumbiji, aliyeongoza nchi hiyo toka 2005 hadi 2015. Armando mwenye miaka 76  ni miongoni mwa washahiri wenye heshima kubwa nchini humo.

Mfano hapa Bongo tungemfananisha na Shaaban Robert au kisasa Mrisho Mpoto na washahiri wengine maarufu akiwa na shahiri lake maarufu la Your Pain ambalo limefanikiwa kutumika katika sekta ya elimu barani Afrika.

JACOB ZUMA

Mwaka 2019, Jacob Zuma ambaye ni rais wa zamani wa Afrika Kusini, amegonga vichwa vya habari za burudani baada ya kutangaza ujio wa albamu yake. Zuma ambaye aliachia madaraka mwezi Februari mwaka jana kwa kashfa ya ufisadi, amewapa ahadi mashabiki zake kuwa ataachia albamu yenye nyimbo zenye maudhui ya mapambano na ukombozi.

Jacob Zuma, alijizolea umaarufu kupitia wimbo  Umshini Wami, ulioamsha hisia za wafuasi wake pindi anapoutumbuiza kwenye majukwaa yake ya kisiasa.

Mkuu wa kitengo cha burudani na masuala ya utamaduni wa mji anaotokea Jacob  Zuma, Durban, KwaZulu-Natal, Thembinkosi Ngcobo, anasema watasimamia albamu hiyo ikiwa ni wazo lao la kufufua nyimbo za zamani ambazo nyingi aliziimba rais huyo, kama mpango wa kuchochea maendeleo na uchumi kupitia muziki, michezo na shughuli za kitamaduni

Rais huyo ambaye tasnia ya burudani Afrika, imekuwa ikimtumia katika mambo ya utani na ucheshi hutumia mitandao ya kijamii, aliyojiunga nayo Disemba 14 mwaka jana kutangaza ujio wa albamu hiyo.

ALI BONGO ONDIMBA

Huyu ni rais wa sasa wa Gabon, ambaye ni mwanamuziki anayeipenda burudani. Amekuwa akipiga ngoma, piano, kutunga na kutengeza nyimbo za Jazz. Ali Bongo amewahi kutengeneza ‘soundtrack’ ya filamu maarufu nchini Gabon,

Mwaka 1977, Ali Bongo alifanya ziara ya muziki nchi nzima ya Gabon aliyoipa jina la Alain Bongo and hisAmerica Orchestra pia alitumbuiza  kwa mtindo wa Hip Hop katika moja ya tamasha kubwa la Gabao Hip hop Festival.

Mwaka 2017, Ali Bongo pamoja na rafiki yake wa siku nyingi ambaye ni nyota wa muziki wa Jazz nchini humo Frédéric Gassita, walimshirikisha Vanessa Mdee kwenye wimbo wao wa pamoja.

“Pale ambapo unafanya muziki na rais, siyo rais wa klabu ni rais wa Gabon,” alitamba Vanessa Mdee alipopata bahati ya kufanya wimbo wa rais Ali Bongo huko jijini Libreville.

Pia Ali Bongo kama mwandaaji wa muziki, ameshiriki kutayarisha albamu nne za rafiki yake huyo mkubwa Frederic Gassica huku kwa pamoja wakitengeneza nyumba ya vipaji yenye mfanano na THT inayoitwa Afro Jazz Productions ambayo inawasaidia wasanii wa nchini humo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles