25.7 C
Dar es Salaam
Saturday, September 21, 2024

Contact us: [email protected]

Mara wataka ulinzi kuimarishwa kukabili ujangili

Na Malima Lubasha, Serengeti

MKUU wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi amewataka askari wanyamapori wa Hifadhi ya Serengeti na Mapori ya Akiba Ikorongo na Grumeti kukabiliana na vitendo vya ujangili na uharibifu wa mazingira ili kulinda ikolojia na viumbe hai.

Kiongozi huyo wa mkoa alikuwa akizungumza katika maadhimisho ya siku ya askari wa wanyamapori Duniani (Word Changer Day –WRD)iliyoandaliwa na Grumeti Fund kwenye viwanja vya kituo cha kutolea elimu ya mazingiraya shirika hilo.

Kanali Mtambi amesema ulinzi wa rasilimali za Taifa ni wajibu wao na kusisitiza kuwa uhifadhi endelevu wa mapori ya akiba Ikorongo- Grumeti, Hifadhi ya Serengeti na Ikona-WMA hauna mbadala, hivyo kuwapongeza askari hao kwa kazi nzuri wanayofanya kulinda maeneo hayo kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Amesema kuwa bila askari hao, wanyamapori ambao ni vivutio vya utalii wakiwemo nyumbu wanaohama wanaweza kupotea na kulisababishia Taifa hasara kwani uhifadhi wa maeneo hayo ni muhimu katika kuingiza fedha za kigeni.

Kanali Mtambi amesema matukio ya ujangili ndani ya maeneo hayo bado yanaendelea huku uharibifu ukijikita kuua wanyama, kuharibu misitu ,vyanzo vya maji na maeneo mengine ya kihifadhi.
Ametoa rai kwa vyombo vya usalama, mamlaka ya uhifadhi na wadau wote kutilia mkazo katika kulinda na kuchukua hatua za kisheria kwa wale wanaofanya vitendo kinyume na sheria kuharibu hifadhi.

Amesema Serikali kupitia mamlaka za uhifadhi kama TAWA na wadau mbalimbali wakiwemo Grumeti wameendelea kusaidia wananchi kuondoa wanyampori wakali na waharibifu hususani tembo katika maeneo yao,kazi hii isipofanyika kwa weledi itasababisha kuongezeka kwa wimbi la majangili kwa kisingizio kuwa mazao yao yameliwa na wanyama hao.

“ Na sisi wahifadhi hatuna budi kuhakikisha tunalinda mashamba ya wananchi waliojirani na hifadhi zetu ili wanyama wasiendelee kuharibu mazao yao,”alisisitiza Kanali Mtambi.

Aidha alitoa onyo kali dhidi ya vitendo vya uharibifu wa mazingira ya bonde la mto Rubana ambao ni sehemu muhimu ya Ikolojia ya Serengeti .

” Mto Rubana ni chanzo muhi mu na lazima kilindwe,alisisitiza na kuzitaka serikali za vijiji vilivyojirani na bonde la mto huo kuanza kuch ukua hatua kali dhidi ya watu wanaoharibu mazingira yam to huo kwa kukata miti na kuchoma mkaa,” amesema.

Hata hivyo Kanali Mtambi alitumia fursa hiyo kumtambulisha Mkuu wa Wilaya mpya wa Serengeti ,Kemirembe Lwota na kumuagiza kusimamia ulinzi wa maeneo ya hifadhi wa wanyamapori .

“DC kwanza karibu Serengeti, nakukabidhi Ikolongo-Grumeti Reserves, Hifadhi ya Serengeti, Ikona-WMA na mto Rubana msipepese macho hata kidogo kwa watu wanaochezea maeneo hayo,” amemueleza DC Kemirembe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles