31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MANJI MGONJWA, ASHINDWA KUFIKA MAHAKAMANI

Na KULWA MZEE-DAR ES SALAAM

MFANYABIASHARA Yusufali Manji (41), ameshindwa kufika mahakamani, baada ya kuelezwa ni mgonjwa na anatibiwa Hospitali ya Magereza Keko.

Manji alishindwa kufika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam jana wakati kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili ilipokuwa inatajwa.

Akiiwakilisha Jamhuri, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Nassoro Katuga, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, alidai upelelezi haujakamilika na kuomba kesi hiyo ipangwe tarehe nyingine.

Katuga, alidai kwa mujibu wa taarifa ya daktari, Manji ni mgonjwa na anatibiwa Hospitali ya Magereza Keko ndiyo sababu kubwa ya kushindwa kufika mahakamani.

Katika kesi hiyo, Manji na wenzake, wanakabiliwa na mashtaka saba chini ya Sheria ya Uhujumu Uchumi na Usalama wa Taifa kwa kukutwa na vitambaa vinavyotengeneza sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vyenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 200 na mihuri.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo, ni Deogratius Kisinda (28), Abdallah Sangey (46) na Thobias Fwere (43). Kesi itatajwa Agosti 4, mwaka huu.

Hati ya mashtaka inayowakabili washtakiwa hao, inadai Juni 30, mwaka huu katika eneo la Chang’ombe ‘A’, Wilaya ya Temeke, Dar es Salaam, kwa pamoja walikutwa na askari polisi wakiwa na bunda 35 za vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare za JWTZ zenye thamani ya Sh milioni 192.5 ambayo ni mali iliyopatikana kinyume cha sheria.

Katika shtaka la pili, inadaiwa Julai mosi, mwaka huu, huko Chang’ombe ‘A’, washtakiwa hao walikutwa na polisi wakiwa na mabunda manane ya vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare hizo yenye thamani ya Sh milioni 44 mali ambayo ilipatikana isivyo halali.

Shtaka la tatu, washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa Juni 30, mwaka huu, Chang’ombe ‘A’, walikutwa na muhuri wa JWTZ wenye maandishi “Mkuu 121 Kikosi cha JWTZ”, bila ya kuwa na uhalali kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.

Katika shtaka la nne, siku hiyo hiyo, eneo hilo la Chang’ombe ‘A’, Manji na wenzake watatu wanadaiwa kuwa walikutwa wakiwa na mhuri wenye maandishi “Kamanda Kikosi 834 KJ Makutupora Dodoma”,  bila ya kuwa na uhalali kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.

Manji na wenzake katika shtaka la tano, wanadaiwa kuwa Juni 30, 2017, huko Chang’ombe ‘A’, walikutwa na mhuri wa JWTZ wenye maandishi “Commanding Officer 835 KJ Mgambo P.0. Box 224 Korogwe”, kitendo ambacho kingehatarisha usalama wa nchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles