31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Manchester City kujiuliza kwa Swansea City EPL

Manchester-City-v-Bayern-MunichLONDON, UINGEREZA

HII inaweza kuwa nafasi nyingine kwa klabu ya Manchester City ya kuongoza Ligi Kuu England kwa tofauti ya mabao ikiwa itaweza kuifunga mabao zaidi ya mawili klabu ya Swansea City.

Hatua hiyo inakuja baada ya kuonekana endapo itafanikiwa kupata alama tatu katika mechi hiyo itafungana kwa alama 32 dhidi ya kinara wa ligi hiyo, Leicester City, hivyo itazilazimu klabu hizo kutofautiana kwa mabao ya kufunga.

Hata hivyo, endapo Manchester City itafanikiwa kupata matokeo mazuri katika mechi hiyo, itakuwa imejinasua katika mfululizo wa awali wa matokeo mabaya ya ligi kuu baada ya kupoteza katika mchezo uliofanyika wiki iliyopita dhidi ya Stoke City.

Upande mwingine Manchester City wanatarajiwa kuanza kwa hali ya juu kutokana na kuweza kupata matokeo mazuri katika michuano ya klabu bingwa Ulaya.

Kwamba  matokeo hayo ya kikosi cha Manuel Pellegrini yamekuja  baada ya kuifunga klabu ya Borussia  Monchengladbach ambapo yanaweza kurudisha hamasa ya mchezo kwa klabu hiyo.

Ikumbukwe klabu ya Swansea ilimfukuza kocha wake, Garry Monk kutokana na matokeo mabaya baada ya kushinda mechi moja katika 11 za ligi kuu.

Msimu uliopita kocha huyo aliweza kuifanya klabu hiyo kukaa nafasi ya nane hadi mwisho wa msimu wa ligi hiyo hivyo kufukuzwa kwake kulionekana kama ghafla.

Garry mwanzoni mwa Septemba mwaka huu akiwa katika kampeni ya ligi kuu England aliweza kupata alama nne baada ya kucheza na kuifunga klabu ya Chelsea pamoja na Manchester United.

James Beattie, ambaye ndiye kocha wa mpito kwa sasa pamoja na msaidizi wake, Pep Clotet, hawana muda mrefu wanaweza kuondoka kiwanja cha Liberty si kwasababu ya mechi ya leo, la hasha, bali ni kutokana na presha za ligi kuu zinazoikabili klabu hiyo.

 

BOURNEMOUTH  VS  MANCHESTER UNITED

BAADA ya kuvurunda katika michuano ya UEFA katikati ya wiki iliyopita, Manchester United inafahamu umuhimu wa kujipanga upya na kuangalia mwelekeo wake katika Ligi Kuu England.

Klabu hiyo ipo nafasi ya nne ikiwa nyuma ya vinara wa ligi hiyo, Leicester City, kwa alama nne na inatarajiwa kuwa katika wakati mgumu wa kupata ushindi dhidi ya wapinzani wake ambao wiki iliyopita waliweza kuifunga nyumbani klabu ya Chelsea bao 1-0.

Mashetani hao bado wanakazana kurudi katika kiwango chao baada ya kupoteza michezo 12 katika michuano yote msimu huu. Lakini kwa sasa ni miezi miwili tangu klabu hiyo ipoteze katika ligi kuu.

Bournemoth imekuwa katika wakati mzuri tangu mchezaji wa klabu hiyo, Wilson kuweka dhamira ya kufanya vizuri tangu Septemba ambapo aliweza kuifungia hat-trick klabu hiyo katika ushindi wa mabao 4-3 dhidi ya West Ham, hivyo anaweza kuufanya mchezo huo kuwa mgumu.

Aston Villa V Arsenal

Kocha wa klabu ya Aston Villa, Remi Garde, bado anaangalia uwezekano wa kupata ushindi wa kwanza akiwa kiongozi wa klabu hiyo dhidi ya aliyekuwa kocha wake wa zamani, Arsene Wenger.

Garde alifanikiwa kukaa misimu mitatu katika klabu ya Arsenal kati ya mwaka 1990 hadi 1998, ambapo aliweza kuondoka katika klabu hiyo.

Pia kocha huyo kabla ya kuondoka alikuwa sehemu ya ushindi wa makombe mawili katika klabu hiyo, akicheza nafasi ya kiungo msimu wa 1997 hadi 98 chini ya kocha Wenger.

Wenger ndiye aliyekuwa kocha wa kwanza kufurahi baada ya Garde kupata kibarua hicho, lakini kibao kinaweza kumgeukia kwa kufungwa na klabu hiyo.

Katika misimu nane ya ligi kuu iliyopita klabu ya Aston Villa hawajawahi kushinda nyumbani, hivyo ili kuweza kulinda heshima yao na kuwafanya wasishuke daraja, ni vema ikapata matokeo kwenye mchezo huo.

Mchezo uliopita klabu ya Watford iliondoka katika kiwanja cha Villa Park na alama zote tatu baada ya kuifunga klabu hiyo mabao 2-3, ambapo kilikuwa kichapo cha 11 kwa Villa kati ya michezo 14 iliyocheza msimu huu.

Mchezo wao mmoja walioshinda msimu huu ilikuwa Agosti dhidi ya klabu ya Bournemouth, lakini waliweza kukaa vizuri na kuonesha kiwango cha kuridhisha kwa kugawana alama walipokwenda ugenini kucheza dhidi ya Southampton.

Kurejea kwa kiungo nyota wa klabu hiyo, Jack Grealish katika kiwanja cha Villa Park kunaweza kuifanya klabu hiyo kuamsha ari ya kupata matokeo mazuri.

Aidha klabu ya Arsenal itashuka katika viwanja vya Villa Park huku ikiwa na kumbukumbu ya kile kilichotokea katika michuano ya klabu bingwa Ulaya.

Ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya klabu ya Olympiakos na kuifanya klabu hiyo kuingia 16 bora.

Olivier Giroud (29) anaonekana kuwa na kiwango kizuri katika msimu huu, lakini je, anaweza kuikata kiu ya klabu hiyo kunyakua ubingwa wa ligi hiyo kwa muda mrefu?

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles