28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mamlaka zahimizwa kushirikiana kutunza vyanzo vya maji bonde la Pangani

Na Safina Sarwatt, Moshi

Bodi ya Maji Bonde la Pangani (PBWB), imezitaka Mamlaka zote za Maji ambazo zinatumia maji kuhakikisha kwamba wanashirikiana na uongozi wa bodi hiyo katika utunzaji wa vyanzo vya maji ikiwa ni pamoja na kuendelea kuotesha miche ya miti kwenye vyanzo vya maji.

Ushauri huo umetolewa Mei 23, 2021 na Afisa Mazingira Bonde la Maji Bonde la Pangani (PBWB), Mhandisi Arafa Maggidi, wakati wa upandaji miti uliofanyika katika Kijiji cha Dakau kitongoji cha Maembe Kata ya Okaoni wilaya ya Moshi kwenye kingo za mto Umbwe.

“Jukumu la usimamizi wa rasilimali za Maji sio la PBWB peke yake, bali ni letu sote, hivyo naziomba Mamlaka za maji zina wajibu wa kusimamia sheria ya utunzaji wa vyanzo vya maji pia,”amesema Mhandisi Maggidi.

Ameongeza kuwa tangu kuzinduliwa kwa Program ya upandaji miti Mei 11, 2021 na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Alhaji Rajab Kundya, jumla ya miche ya miti 10,000 imepandwa kwenye kingo za mito, chemi chemi za maji pamoja vyanzo vya maji.

“Tangu kuzinduliwa kwa program hii ya upandaji wa miche ya miti, jumla ya miti 10,000, tumeipanda kwenye kingo za mito, chemi chemi na kwenye vyanzo vya maji, lengo ni kuhakikisha kwamba vyanzo vyote vya maji vinaendelea kuwepo,” amesema Mhandisi Maggidi.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, Peter Tete, amewataka wananchi kuzingatia sheria zilizopo za utunzaji wa vyanzo vya maji kwa hiari pasipo kuilazimisha serikali kutumia nguvu.

Amesema ili kuwe na vyanzo endelevu vya maji ni lazima wananchi wavitunze vyanzo vya maji na sheria ya kukaa umbali wa mita 60 kutokea mtoni inazingatiwa na kwa wale ambao watakaidi serikali itawachukulia hatua kali za kisheria

“Kuna baadhi watu wanaoharibu vyanzo vya maji kwa kufanya shughuli za kilimo, kuponda kokoto, kulisha mifugo haya yote yanachangia uharibifu na kusababisha ukosefu wa maji hasa wakati wa kiangazi,” amesema Tete.

Aidha, amewataka wananchi kuhakikisha kuwa vyanzo vyote vya maji vinatunzwa na kulindwa kwa kuendelea kupandwa miti maalumu inayohifadhi maji na kwa wale wanaofanya shughuli za binadamu kwenye vyanzo vya maji kuacha tabia hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles