27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

MAMANTILIE WAPANDISHA BEI YA CHAKULA

TUNU NASSOR Na FERDNANDA MBAMILA-DAR ES SALAAM

WAUZAJI wa chakula Dar es Salaam, maarufu mamantilie au mamalishe, wamepandisha bei ya chakula ili kukabiliana na mfumuko wa bei za nafaka.

Mbali na kupandisha bei, wamelazimika kupunguza kipimo cha chakula kutokana na kupanda kwa bei za nafaka katika masoko mbalimbali.

Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA jana katika masoko ya Tandale, Mabibo na Magomeni, umebaini kuwa sahani moja ya ugali na mboga za majani inauzwa kati ya Sh 1,500 na 2,000 badala ya Sh 1,000 hadi 1,200, huku ugali mkavu ukiuzwa kwa Sh 1,500.

Wakizungumza na MTANZANIA kwa nyakati tofauti jana, baadhi ya mamalishe wa soko la Tandale na Magomeni, walisema wameamua kuongeza bei ili kuendana na bei za vyakula ambavyo vimeendelea kupanda kila siku.

Mmoja wa mamalishe katika soko la Magomeni, Hellen Mwita, alisema endapo bei zitaendelea kupanda, watalazimika kuigawa sahani moja ya ugali mara mbili.

“Kwa sasa tumepunguza kipimo cha chakula na kuongeza bei kwa sahani moja, lakini hali bado si nzuri na ikizidi kuwa mbaya tutalazimika kugawa sahani moja mara mbili,” alisema Hellen.

Alisema hata hivyo, biashara imekuwa ngumu kwa kipindi hiki ukilinganisha na ilivyokuwa mwaka jana na mwaka juzi, kutokana na bei kupanda hivyo wanahofu ya kupoteza wateja.

“Wateja wetu kwa sasa wamepungua, wengi wanadai kuwa bei ni kubwa, lakini chakula tunachowapa ni kidogo,” alisema Hellen.

Naye Mariamu Abdul ambaye anafanyia shughuli zake katika Soko la Tandale, alisema imewabidi kuongeza bei na kupunguza kipimo kutokana na ongezeko hilo.

“Pamoja na kupandisha bei na kupunguza kipimo cha chakula, faida tunayoipata ni ndogo tofauti na miaka iliyopita,” alisema Mariamu.

Bei za bidhaa zapaa

Katika Soko la Tandale, bei ya mahindi imepanda kutoka wastani wa Sh 75,000 hadi 120,000 kwa gunia moja la kilo 100, huku mtama ukipanda kutoka Sh 60,000 hadi kufikia 100,000 kwa gunia la kilo 100.

Mfuko wa unga wa mahindi wenye kilo 25 ambao awali ulikuwa ukiuzwa kwa Sh  22,000, hivi sasa unauzwa kwa Sh 35,000.

Katika Soko la Mabibo, maarufu ‘Mahakama ya Ndizi’, viazi mbatata vimepanda kutoka Sh 1,000 kwa kilo moja hadi kufikia 1,500, huku ndoo moja ikiuzwa Sh 16,000.

Katika soko hilo, mkungu mmoja wa ndizi mshale na zile za Bukoba zinauzwa kati ya Sh 16,000 hadi 22,000 kulingana na ukubwa wa mkungu, huku mikubwa zaidi ikiuzwa kati ya Sh 25,000 na 35,000.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles