24.3 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

MAMA LISHE WAWATUHUMU MAOFISA AFYA KUWAOMBA FEDHA

Na TWALAD  SALUM

MAMA lishe wa Kata ya Misungwi wilayani Misungwi   wamemlalamikia Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya hiyo,   Ackim Jackson,  kuhusu     baadhi ya maofisa afya wa kata hiyo  wanaowaomba  kati ya Sh 3,000 na Sh 5,000    kwa ajili ya kuwapima afya .

Walikuwa wakizungumza juzi wakati  ziara ya siku mbili ya Katibu wa CCM wilaya hiyo  kwenye  Kata na Kijiji cha Misungwi  kwenye ukumbi wa Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Misungwi

Baadhi ya  mama lishe hao ni wanaofanya shughuli zao katika soko kuu la Misungwi na soko la zamani .

Kwa mujibu wa kina mama hao, hutoa fedha za kupimwa afya zao bila kupatiwa huduma hiyo

Walisema wamekuwa  wakitoa fedha  kati ya Sh 3,000 na Sh 5,000 mara kwa mara kwa maofisa afya kwa ajili ya kupimwa afya zao lakini hawawapati huduma hiyo    jambo ambalo   wameliona kuwa ni   rushwa kwa maofisa hao.

Mama lishe wa Soko la Zamani,  Ester Samson,  alisema maofisa afya wamekuwa wakipita sehemu wanazofanyia biashara zao wakiwa na daftari na kuwachangisha  kati ya Sh  3,000 na Sh 5,000 na kuwaandika majina yao kwa ajili ya kupimwa afya.

“Tunaomba chama tawala kitusaidie kuna maofisa afya wawili hupita mara kwa mara wakituchangisha fedha na usipotoa wanakufungia biashara yako…  sisi tuna watoto wanategemea kama mimi ni  mjane mtusaidie tumegeuzwa Saccos,” alisema Ester Samson.

Naye Mariam John alsema kuna Ofisa Afya mmoja    ambaye huwavizia asubuhi   na akiwakuta hawajavaa sare anaomba sare ambazo hazijavaliwa na kuzichukua ili awalipishe faini.

“Wengine  hutuvizia mapema,  akikukuta unasukuma chapati umevaa kofia tu anachukua aproni unayotarajia kuivaa na kuondoka nayo ili aje baadaye akutoze faini ya Sh 50,000 … atakupa namba ya akaunti ya benki ya NMB ukalipie usipofanya hivyo anakufungia biashara,”  alisema  John.

Hata hivyo,  Ofisa Afya  ya Jamii wa Kata  ya Misungwi, Paulina Kubimbi,  alisema alikumbana  siku moja na  mama lishe ambaye alimpa Sh 1,000 kwa ajili ya soda na aliomba amrudishie.

“Tulikuwa na Mary tukapita kwa mama lishe huko bondeni akatupa Sh 1,000 ya soda, kama hiyo ni rushwa ntamrudishia asitupake matope sisi ni maofisa,” alisema Kubimbi.

Abubakari Abdallah,  aliyetuhumiwa kuchukua sare zao na kuondoka nazo kwa lengo la kuwatoza faini,  alisema amekuwa akitumia busara kwa wale wanaoshindwa kufuataSsheria za Afya ya Jamii kwa kuvaaa sare.

Alisema amekuwa akiwanyang’anya sare ambazo huwa wamezining’iniza bila kuzivaa ili wapate uchungu wazivae na wale wanaodai huwatoza  faini ya Sh 50,000.  Alikiomba chama kimuunge mkono.

“Nakiomba chama kiniunge mkono badala ya kunikatisha tamaa kwa sababu  mimi naogoza wilaya hii kuingiza pato kwa kuwatoza faini nimeingiza zaidi ya Sh milioni mbili  kwa mwaka huu,  lengo ni kuwataka  kufuata sheria ya afya,” alisema Abdallah.

Katibu wa CCM wa Wilaya, Jackson aliwataka watendaji kufanya kazi  zao kwa kutowaonea wananchi  na mama lishe akawashauri watimize  masharti  ya usafi   kuepuka magonjwa ya mlipuko.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles