26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mama Diamond akimtambua vizuri mwanaye atampenda sana Zari

mama-diamond-n-zariMWAKA 2009 Diamond Plutnumz akiwa ndiyo kwanza ameingia katika ulimwengu wa umaarufu, alihojiwa na jarida fulani maarufu ambalo kwa sasa halitoki tena juu ya matarajio yake katika muziki na maisha.

Japo kwa nyakati zile wengi huenda hawakumuelewa, ila Diamond alisema kuwa, dhamira yake ya kwanza anataka kuwa mwanamuziki maarufu sana Afrika halafu awe mwanamuziki tajiri.

Kutoka mwaka 2009 mpaka sasa siyo miaka michache. Katika yale aliyoongea Diamond kuna picha kubwa ya kweli inakuja katika akili ya kila mdau wa kweli wa Bongo Flava.

Kuna kila dalili ya Diamond kuishi ndoto yake kama Mungu akizidi kumpa uhai na ukumbusho wa dhamira yake. Ila wakati mwingine ndoto katika maisha siyo kitu cha kushangaza sana.

Kila mmoja ana ndoto yake. Kuna wanamuziki walikuwa na ndoto kama za Diamond na wengine zaidi yake ila wengi wamekata tamaa na wengine wakaona kama ni ujinga kuwaza hivyo.

Msingi wa ndoto katika maisha ni mikakati ya namna ya kuifikia. Katika hili kuna somo hapa kwa Diamond. Mbali na jitihada zake za usiku na mchana na kuwa na timu kubwa ya uongozi yenye watu makini na  uelewa wa kutosha kuhusiana na muziki wa nyumbani na wa kimataifa.

Hapa nawazungumzia watu kama Said Fella, Babu Tale, Salami, Ruge Mutahaba nk. Katika akili ya kawaida ukiwa na watu hawa na kuwasikiliza kwa makini na kutumia akili yako vyema, una nafasi kubwa sana ya kuwa msanii mzuri.

Ila kando na hivyo, Diamond anaonekana kuwaza nje ya sanduku (to think outside the box) kitu ambacho wanamuziki wengi wanashindwa.

Diamond katika kufikia ndoto yake anaangalia anakaa na nani, marafiki zake ni akina nani na mwisho ni nani anayelala naye kitanda kimoja na kumuita mpenzi au mke wake.

Hapa ndiyo kuna kitu ambacho mama Diamond, dada yake Diamond na wengine wanapaswa kuelewa. Toka zamani imetajwa, nyuma ya mafanikio ya kila mwanaume kuna mwanamke makini.

Hapa Diamond ndipo karata yake ya ushindi huenda inapopatikana. Mwenyewe aliwahi kuandika katika mitandao ya kijamii kuhusiana na mahusiano yake na Wema Sepetu.

Mbali na kuandika mengi ila pointi zake zilieleza kuwa Wema wa kipindi kile (sijui wa sasa) alikuwa anawaza sana starehe na sifa. Kwa maelezo yake ni kuwa wakati watu wakimlaumu kuwa eti anatumia nyota ya Wema kufanya vizuri katika biashara yake ya muziki, Wema mwenyewe alikuwa hana muda na filamu zake zaidi ya starehe na kutafuta sifa za kuitwa tajiri hali hana kitu.

Alipoachana na Wema na kuingia katika mahusiano na mwanadada mrembo, makini na mfanyabiashara, Zarina Hassan ‘Zari the boss Lady’, Diamond aliwahi tena kukiri kuwa toka awe na mrembo huyo kutoka Uganda hata mtazamo wake kimaisha na kibiashara umebadilika na kukua zaidi.

Hapa ndipo kuna somo halisi. Zari ni zaidi ya mwanamke kwa Diamond. Zari ni mshauri, mama wa watoto na dira yake ya kimafanikio ya jabali huyo wa Tandale.

Mtu mwingine kwa sababu zake za Kiswahili anapotamani Zari na Diamond waachane, kwa sababu yoyote ile, hajui kuwa maumivu na madhila ya wawili hawa kuachana siyo ya Zari pekee ila yatamgusa kwa kiwango kikubwa na Diamond mwenyewe.

Watu wajifunze kutoka kwa akina Tiger Wood na wengineo. Baada ya mwanamichezo huyo kuachana na mke wake hata ufanisi wake katika michezo ukashuka na akayumba sana kiuchumi.

Rai yangu ni kuwa, kama mama Diamond ana uhasama au chuki yoyote binafsi na Zari, inabidi afahamu mwanaye amependa na anafaidika kiakili na kimwili kwa binti huyo.

Hiyo misuguano inayosemwa naona haina maana kabisa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles