
Na YASSIN ISSAH, DAR ES SALAAM
MKAZI wa Yombo Dovya, Dar es Salaam, Rehema Saidi, ameomba msaada wa matibabu na baiskeli ya walemavu kwa mwanae, Zuhura Seki mwenye ulemavu wa viungo kwa takriban miaka 10 sasa.
Akizungumza na MTANZANIA nyumbani kwao Yombo Dovya, Rehema alidai alitelekezwa na mume wake kwa miaka mitano baada ya kujifungua mtoto mlemavu ambaye anaishi naye kwa baba yake mzazi huko Yombo.
“Matatizo yalianza baada ya miaka mitatu nilipojifungua mtoto huyu akiwa mlemavu wa viungo.
“Baba wa mtoto huyu alianza kubadilika, akawa hatumi fedha za matumizi akidai hawezi kumhudumia mtoto mlemavu, akisema kuwa si wa kwake,” alisema Rehema.
Alisema kuwa kabla ya Yombo, alikuwa akiishi Rufiji mkoani Pwani na alifika Dar es Salaam kwa ajili ya kupata matibabu ya upasuaji wa tumbo kutokana na uvimbe.
Rehema alisema kuwa alipata matibabu hayo na hivi sasa anaendelea vizuri.
“Kilichonifanya kuja Dar es Salaam ilikuwa ni kwa ajili ya kupata matibabu kwa vile ilionekana nina uvimbe katika tumbo, lakini sikuwa na fedha za matibabu ila kaka yangu ndiye aliyenisaidia ikizingatiwa matibabu yalihitaji Sh 100,000,” alisema.
Mama huyo anaomba msaada wa makazi ikiwa ni pamoja na huduma ya matibabu kwa mtoto wake.
“Kwa sasa naishi kwa baba yangu mzazi, Mzee Saidi Mkingie, lakini pia hali ya maisha ya baba yangu ni ngumu… hana uwezo wowote, ninaomba msaada wenu Watanzania wenzangu kwa sababu sina pa kukimbilia,” alisema.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Yombo, Bruce Mbagwile, alisema awali hakuwa na taarifa ya kuwapo tatizo hilo mtaani kwake.
Hata hivyo aliahidi kukaa na kamati inayoshughulikia watoto wanaoishi mazingira magumu, kitengo cha walemavu, kuona watamsaidia vipi mtoto huyo aweze kusoma.
“Tutakaa na kamati kuangalia tutamsaidia vipi mtoto huyu aweze kusoma katika Shule ya Msingi Dovya ambayo ina kitengo cha walemavu,” alisema